JE, UMEWAHI kuona jinsi ambavyo watoto huuliza maswali? Wengi wao huanza kuuliza maswali mara tu wanapojua kuongea. Wanakutazama wakiwa wamekodoa macho kwa hamu na kuuliza maswali kama vile: Kwa nini anga ni bluu? Kwa nini nyota zinametameta? Ni nani aliyewafundisha ndege kuimba? Huenda ukajaribu sana kujibu, lakini mara nyingi si rahisi. Hata baada ya kuwapa jibu bora, huenda bado wakauliza: Kwa nini?
1. Kwa nini ni vizuri kuuliza maswali?
 Si watoto peke yao wanaouliza maswali. Tunapoendelea kukua, sisi huuliza maswali. Tunauliza maswali ili tupate mwongozo, tujue hatari tunazohitaji kuepuka, au kwa sababu tu tunataka kujua. Hata hivyo, inaonekana kwamba watu wengi huacha kuuliza maswali, hasa yaliyo muhimu zaidi. Wao huacha kutafuta majibu.
2. Kwa nini watu wengi hawajitahidi kupata majibu ya maswali muhimu zaidi?

Fikiria swali lililo katika jalada  la kitabu hikimaswali yaliyo katika utangulizi wa kitabu hiki, au  yale yaliyo mwanzoni mwa sura hii. Hayo ni baadhi ya maswali muhimu zaidi unayoweza kuuliza. Hata hivyo, watu wengi hawajitahidi kupata majibu ya maswali hayo. Kwa nini? Je, Biblia ina majibu? Watu fulani hufikiri kwamba Biblia haieleweki. Wengine huogopa kuuliza maswali ili wasiaibishwe au kudharauliwa. Hali wengine huamua kwamba maswali hayo yanaweza kujibiwa tu na viongozi na walimu wa dini. Wewe unaonaje?
Yesu anakupenda. Yeye ni njia ya kweli na Uzima hakuna ajaye kwa Mungu pasipo kumfuata Yesu Kristo.3. Ni maswali gani muhimu zaidi tunayoweza kuuliza maishani, na kwa nini tutafute majibu?

Bila shaka ungependa kupata majibu ya maswali muhimu zaidi maishani. Haikosi, nyakati nyingine wewe hujiuliza: ‘Maisha yana kusudi gani? Je, kusudi pekee la maisha ni kuzaliwa, kuzeeka, na kufa? Kwa kweli Mungu ana utu gani?’ Ni vizuri kuuliza maswali kama hayo, na ni muhimu kutafuta majibu yenye kuridhisha na yenye kutegemeka bila kukata tamaa. Yule mwalimu mashuhuri, Yesu Kristo, alisema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.”Mathayo 7:7.
Ukiendelea kutafuta’ majibu ya maswali hayo muhimu, utafaidika sana. (Methali 2:1-5) Hata uwe umeambiwa nini na watu wengine,kuna majibu, na unaweza kuyapata katika Biblia. Majibu hayo si magumu, yasiyoeleweka. Isitoshe, yatakupa tumaini na shangwe. Na yanaweza kukusaidia kuishi maisha yenye kuridhisha sasa. Kwanza, na tufikirie swali moja ambalo limewahangaisha watu wengi.
4. JE, MUNGU ANA HURUMA NA JE, ANAJALI?
Kwa nini watu wengi wanafikiri kwamba Mungu hajali wanadamu wanapoteseka?
Watu wengi hujibu hapana. Wanasema, ‘Ikiwa Mungu anajali, ulimwengu ungekuwa tofauti sana.’ Leo, ulimwengu umejaa vita, chuki, na mateso. Isitoshe, kila mmoja  wetu huwa mgonjwa, huteseka, na kufiwa na wapendwa wake. Ndiyo sababu watu wengi husema, ‘Ikiwa Mungu anatujali na kuhangaikia matatizo yetu, kwa nini hazuii mambo hayo yasitupate?’
(a) Walimu wa dini wamewafanyaje watu wengi wafikiri kwamba Mungu hana huruma? (b) Biblia inafundisha nini hasa kuhusu majaribu ambayo huenda yakatupata?
Isitoshe, nyakati nyingine walimu wa dini huwafanya watu wafikiri kwamba Mungu hana huruma. Jinsi gani? Msiba unapotokea, wanasema ni mapenzi ya Mungu. Kwa kweli, walimu hao wanamlaumu Mungu kwa sababu ya mambo mabaya yanayotukia. Je, huo ndio ukweli kumhusu Mungu? Biblia inafundisha nini hasa? Andiko laYakobo 1:13 linajibu: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” Kwa hiyo, Mungu hasababishi kamwe uovu ambao unaona ulimwenguni. (Ayubu 34:10-12) Ni kweli kwamba anaacha mambo mabaya yatukie. Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kuacha jambo litukie na kulisababisha.
5. Unaweza kutumia mfano gani kuonyesha tofauti iliyopo kati ya kuacha uovu uwepo na kuusababisha? (b) Kwa nini si haki kumlaumu Mungu kwa kuwaacha wanadamu wafuate njia isiyofaa?
Kwa mfano, wazia baba mwenye hekima na busara aliye na mwana ambaye tayari ni mtu mzima na bado anaishi nyumbani kwa wazazi wake. Mwana huyo akiasi na kuamua kuondoka nyumbani, baba yake hamzuii. Mwana huyo anaishi maisha mapotovu na kupata matatizo. Je, baba ndiye aliyesababisha matatizo ya mwanaye? Hapana. (Luka 15:11-13) Vivyo hivyo, Mungu hawazuii wanadamu wakishaamua kufuata njia isiyofaa, hata hivyo hasababishi matatizo yanayowapata. Kwa hiyo, basi, si haki kumlaumu Mungu kwa sababu ya matatizo yote yanayowapata wanadamu.

Mungu ana sababu nzuri za kuwaacha wanadamu wafuate  njia isiyofaa. Akiwa Muumba wetu mwenye hekima na nguvu, hahitaji kutueleza sababu hizo. Hata hivyo, Mungu hutueleza kwa sababu ya upendo. Utajifunza kuhusu sababu hizo katika Sura ya 11. Lakini uwe na hakika kwamba Mungu hasababishi matatizo yanayotupata. Badala yake, anatupa tumaini pekee la utatuzi!—Isaya 33:2.
6. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu ataondoa madhara yote      yanayotokana na uovu?
Isitoshe, Mungu ni mtakatifu. (Isaya 6:3) Hilo linamaanisha kwamba yeye ni safi wala hana uovu hata kidogo. Kwa hiyo, tunaweza kumtumaini kabisa. Hatuwezi kuwatumaini wanadamu ambao nyakati nyingine wanakuwa wafisadi. Hata wanadamu wenye mamlaka ambao ni wanyoofu zaidi mara nyingi hawana uwezo wa kuondoa madhara yanayosababishwa na watu wabaya. Lakini Mungu ana nguvu zote. Anaweza na ataondoa madhara yote yanayowapata wanadamu kwa sababu ya uovu. Mungu atakapochukua hatua, atakomesha uovu milele!—Zaburi 37:9-11.
MUNGU ANAHISIJE KUHUSU UKOSEFU WA HAKI?
7. Mungu anahisije kuhusu ukosefu wa haki? (b) Mungu anahisije kuhusu kuteseka kwako?
Mungu anahisije kuhusu mambo yanayoendelea ulimwenguni na maishani mwako? Kwanza kabisa, Biblia inafundisha kwamba Mungu ni “mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Kwa hiyo anapendezwa sana na mambo yanayofaa na kuchukizwa na mambo yasiyofaa. Anachukia ukosefu wa haki wa kila namna. Biblia inasema kwamba Mungu ‘aliumia moyoni mwake’ uovu ulipokuwa mwingi duniani wakati uliopita. (Mwanzo 6:5, 6) Mungu hajabadilika.
(Malaki 3:6) Bado anachukia kuona mateso yanayoendelea ulimwenguni pote. Pia, Mungu anachukia kuona watu wakiteseka. Biblia inasema, “yeye anawajali ninyi.”—1 Petro 5:7.
Biblia inafundisha kwamba Yehova ni Muumba wa ulimwengu mwenye upendo
8. Kwa nini tuna sifa nzuri kama vile upendo, nao upendo unatufanya tuwe na maoni gani kuhusu ulimwengu? (b) Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atachukua hatua kuhusiana na matatizo ya ulimwengu?
Tunawezaje kuwa na hakika kwamba Mungu anachukia kuona watu wakiteseka? Uthibitisho mwingine ndio huu. Biblia inafundisha kwamba Mungu alimuumba mtu kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Kwa hiyo, tuna sifa nzuri kwa sababu Mungu ana sifa nzuri. Kwa mfano, je, wewe husumbuka unapowaona watu wasio na hatia wakiteseka? Ikiwa unasumbuka kwa sababu ya ukosefu huo wa haki, uwe na hakika kwamba Mungu husumbuka hata zaidi.

Jambo moja la pekee kuhusu wanadamu ni kwamba tuna uwezo wa kuonyesha upendo. Mungu pia ana sifa hiyo. Biblia inafundisha kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Tuna upendo kwa sababu Mungu ana upendo. Je, upendo ungekuchochea kukomesha mateso na ukosefu wa haki unaoona ulimwenguni? Kama ungekuwa na uwezo wa kufanya hivyo, je, ungeyakomesha? Bila shaka ungeyakomesha! Uwe na hakika kwamba Mungu atakomesha mateso na ukosefu wa haki. Ahadi zinazotajwa katika utangulizi wa kitabu hiki si ndoto tu au matumaini yasiyo na msingi. Bila shaka ahadi za Mungu zitatimia! Hata hivyo, ili kuamini ahadi hizo, unahitaji kujua mengi zaidi kumhusu Mungu anayezitoa.


Share To:
Magpress

Calvin Petro

Kwa Moyo wangu wote nimekutafuta, Usiniache nipotee mbali na Maagizo yako. Moyoni mwangu nimeliweka Neno lako Nisije nikakutenda dhambi. (Zaburi 119:10-11).

Post A Comment:

0 comments so far,add yours