Hatua ya kuweka akiba, ni matokeo ya maamuzi. Akiba ni matokeo ya maamuzi ya kuweka vitu sasa, kwa ajili ya kuvitumia baadaye. Ukiona mtu anaweka akiba, ujue anatekeleza maamuzi yake, yanayogusa nyakati mbili za Maisha, nyakati ya sasa na nyakati ya baadaye.


Kwa hiyo, haina maana ya kwamba, vitu unavyoamua kuviweka akiba sasa, kwa ajili ya kuvitumia baadaye, huna kazi navyo sasa – la hasha! Lakini sababu ya kutumia vitu hivyo baadaye, ni kubwa kiumuhimu, kuliko sababu ya kuvitumia sasa!
Hebu tujifunze zaidi juu ya hekima hii, kwa kuangalia mifano ifuatayo:
Mfano 1: Sababu zilizomfanya Mfalme Daudi aweka akiba.


Ukisoma 1 Mambo ya Nyakati 29:2 utaona mfalme Daudi akisema hivi: “nimeiwekea akiba nyumba ya Mungu wangu…”. Sababu yake ya kuiwekea akiba nyumba ya Mungu, tunaipata tunaposoma alichosema mfalme Daudi kwenye 1 Mambo ya Nyakati 29:3, aliposema hivi: “Nami tena kwa kuwa nimeiwekea nyumba ya Mungu wangu shauku yangu…”


Mfalme Daudi alitaka waliokuwa wanamsikiliza, wajue ya kuwa, vitu alivyoviweka akiba kwa ajili ya nyumba ya Mungu, aliviweka akiba, si kwamba hakuwa na shida wakati ule, iliyohitaji matumizi ya vitu vile. La hasha!
Ila “Shauku” au “Sababu” ya kuona nyumba ya Mungu wake inajengwa, ilikuwa kubwa kiumuhimu, kuliko kuvitumia wakati ule. Na tena – hakutaka mrithi wake yaani Sulemani, aliyepewa jukumu la kuijenga nyumba hiyo, aje awe na tatizo katika kupata vitu vya kuanzia kuijenga nyumba ile.


Mfalme Daudi alisema “katika shida yangu, nimeiwekea akiba nyumba ya Bwana…” (1 Mambo ya Nyakati 22:14). Hii inaonyesha ya kuwa alifanya maamuzi ya kuweka akiba akiwa katika mazingira ya “shida”. Lakini moyoni mwake kulikuwa na Shauku kubwa ya kuona nyumba ya Mungu wake inajengwa, kiasi cha kuishinda sauti ya “shida” iliyokuwa “inalia” moyoni mwake, kutaka kutumia vitu vile vile alivyoamua kuviweka akiba!


Je, ndani ya moyo wako kuna shida inayolilia kuvitumia vitu ulivyonavyo, ambavyo pia ulitaka kuviweka akiba kwa ajili ya kuvitumia baadaye? Je, ni sauti ipi inayoshinda? Ni ile ya kuvitumia katika shida uliyonayo sasa, au ni ile inayotaka uviweke akiba kwa ajili ya kuvitumia “baadaye”?
Je, unaweza kuikubali “hekima” hii ya mfalme Daudi? Pamoja na shida aliyokuwa nayo, wakati ule alipokuwa anaweka akiba, aliona ni vema kuweka akiba, kuliko kumaliza alichokuwa nacho katika kushughulikia shida aliyokuwa nayo! Unasemaje katika hili?
Mfano wa 2: Sababu inayomfanya mdudu Chungu kuweka akiba ya chakula wakati wa joto.


Biblia inasema “Ewe mvivu, mwendee Chungu, zitafakari njia zake upate hekima…hujiwekea akiba ya chakula wakati wa jua; hukusanya chakula chake wakati wa mavuno” (Mithali 6:6,8).
“Chungu” anayetajwa hapa ni aina ya sisimizi, au aina ya siafu. Biblia inatuambia ya kwamba”hujiwekea akiba ya chakula” wakati wa joto. Kwa nini anafanya hivyo?
Ni kwa sababu anajua ya kuwa kipindi cha joto ni kipindi cha mavuno ya chakula anachokula, ambacho hakipatikani wakati wa baridi, kwa kuwa kipindi cha baridi si kipindi cha mavuno ya chakula chake!
Hii inatupa kujua ya kuwa, “Sababu” za mdudu Chungu kuweka akiba ya chakula wakati wa joto, ni kubwa kiumuhimu, kuliko kukila chakula chote wakati alipokuwa anakikusanya. La sivyo, wakati wa baridi hatakuwa na chakula cha kula, kwa kuwa hakuna mavuno ya chakula chake wakati wa baridi.


Tungelitazama jambo hili kimapato, tungejua ya kwamba kipindi cha joto kilikuwa kipindi cha kupata kipato chake, na kipindi cha baridi ni kipindi ambacho hana kipato. Uamuzi aliokuwa nao si kutumia kipato chake chote alichokipata wakati wa joto, bali aliamua baadhi ya kipato chake akiweke akiba, ili aje akitumie wakati hana kipato – yaani wakati wa kipindi cha baridi!
Je, maamuzi yako unayofanya juu ya kipato unachopata yakoje? Unatumia kipato chote kwa matumizi yako ya sasa au kuna baadhi ya kipato unachokiweka akiba kwa ajili ya matumizi ya baadaye?


Endelea kufuatana nasi kwenye mfululizo wa somo hili , hapa kwenye ukurasa wetu wa facebook katika siku chache zijazo.
Mungu aendelee kukubariki , na tuzidi kuombeana. 





Image result for Mwalimu mwakasege


Share To:
Magpress

Bila jina

Kwa Moyo wangu wote nimekutafuta, Usiniache nipotee mbali na Maagizo yako. Moyoni mwangu nimeliweka Neno lako Nisije nikakutenda dhambi. (Zaburi 119:10-11).

Post A Comment:

0 comments so far,add yours