Bila ya kuwa na maono ya wapi unaelekea ni rahisi kuchukuliwa na upepo na kupelekwa usikokutazamia. Maono yatakufanya ujue ni nini ufanye kwa ajili ya Mungu na maisha yako kwa ujumla.

Mithali 29: 18 

Maono yako kwa ajili ya kazi ya Mungu ni lazima yaendane na agizo kuu alilolitoa Bwana Yesu kwa wote wanaomwamini.

Marko 16:15 Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri injili kwa kila kiumbe.

Ni lazima mara zote agizo hili liwe ndani yako ili unapoendelea na maono yako usijeenda mbali na agizo hili.

Shetani hujaribu kuyafisha maono yako na usipokuwa mwangalifu atayapoteza kabisa. Yeye mara zote hutaka kituzuia kuyafanya mapenzi ya Mungu, anajua akiyaua maono yetu hatutaweza kuifanya kazi ya Mungu kwa ukamilifu.

2Korintho 2:11 Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake.

Mambo yafuatayo shetani huyatumia kuua maono yetu:

1. Dhambi ambazo hazijatubiwa
Isaya 59:9-12 Mistari hii inaonyesha kuwa dhambi isipotubiwa hupofusha macho ya rohoni hivyo hutaweza kuyaona maono yako. Dhambi inakuweka mbali na utukufu wa Mungu.

2. Uhusiano uliovinjika katika mwili wa Kristo 
Tunaporuhusu makosa ya ndugu zetu katika Kristo kuzaa uchungu badala ya kusamehe, tunaruhusu shetani kuyafunga macho yetu ya kiroho na hivyo kushindwa kuiona njia ya kuelekea kwenye maono yetu.

3. Tamaa ya mambo yanayoonekana

Zaburi 119:37 Unigeuze macho yangu nisitazame yasiyofaa, unihuishe katika njia yako.

Ukiangalia sana mambo ya dunia na tamaa zake utajikuta unayasahau maono yako na kubaki umefungwa na mambo hayo.

4. Kuangalia sana mambo ya nyuma.

 Unapoacha kutazama mbele unapoelekea na kuweka nguvu na akili yako yote katika mambo ya nyuma yaliyopita, utapoteza kusudi lako na maono yako.

Mwanzo 19:26 Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi.

Wafilipi 3:13 Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele.

5. Kutumia muda mwingi kuangalia matatizo

Shetani hujaribu kutufanya tuangalie tu matatizo tuliyonayo na yale yanayoweza kutokea tunapoyafanyia kazi maono yetu hivyo kutuondolea imani ya kuyakamilisha. Biblia katika kitabu cha hesabu inaelezea habari za wapelelezi kumi waliorudi na habari za kukatisha tamaa katika kuiendea nchi ya ahadi maana waliangalia zaidi matatizo na kupoteza maono yao ya kuingia nchi ya ahadi.

Joshua na Kaleb waliona zaidi ya matatizo, waliuona ukuu na uaminifu wa Mungu. Hawakuwa na hofu yoyote hivyo waliweza kuingia nchi ya ahadi (kukamilisha maono yao) maana walimwamini Mungu. Petro alijaribu kutembea juu ya maji lakini alipoona mawimbi akasahau Yesu aliyekuwa mbele yake akimwambia njoo, akaweka akili kwenye mawimbi akaanza kuzama.

Ili tuweze kuyafanikisha maono yetu ni lazima tuwe na uhusiano na ushirika wa karibu na Roho Mtakatifu.

Ubarikiwe na BWANA Yesu.




 chanzo: https://womenofchrist.wordpress.com

Share To:
Magpress

Calvin Petro

Kwa Moyo wangu wote nimekutafuta, Usiniache nipotee mbali na Maagizo yako. Moyoni mwangu nimeliweka Neno lako Nisije nikakutenda dhambi. (Zaburi 119:10-11).

Post A Comment:

0 comments so far,add yours