Top News



Mwaka 1997 tulipokea barua na simu nyingi toka kwa watu wa Mungu mbalimbali wakihitaji maombi kwa ajili ya matatizo yaliyokuwa yanawasumbua katika maeneo ya kifedha. Wengine biashara na kazi zao vilikuwa haviendi vizuri - nakadhalika.
Tulikaa na jambo hili katika maombi. Tarehe 24 Septemba 1997 saa kumi na nusu asubuhi tukiwa katika maombi Bwana Yesu alisema nasi katika mioyo yetu ujumbe ufuatao ambao tunaamini utakusaidia hata wewe. Bwana Yesu alituambia hivi:


roho ya mpinga Kristo ndiyo iliyoshambulia mafanikio ya kifedha katika watu wangu,

Imeelekeza mashambulizi katika mafanikio ya roho zao (na nafsi zao) maana nimesema mtafanikiwa katika mambo yote kwa kadri roho zenu zifanikiwavyo,

Kufanikikiwa kwa roho zenu kunategemea kufanikiwa kwa nafsi zenu. Mtafanikiwa katika roho zenu kwa kadri nafsi zenu zifanikiwavyo, na matokeo yataonekana katika mambo yote

Nafsi zenu zifanikiwavyo zinategemea utendaji wenu wa Neno langu. Ikiwa utendaji wenu wa Neno ukiwa hafifu, na kufanikiwa kwa nafsi zenu kunakuwa hafifu. Kufanikiwa kwa nafsi zenu kukuwa hafifu na kufanikiwa kwa roho zenu kunakuwa hafifu, kwa hiyo kufanikiwa katika mambo yote kunakuwa hafifu pia.

Ndiyo maana nasema roho ya mpinga Kristo imeelekeza mashambulizi yake katika kupinga, kuzuia, na kuchelewesha mafanikio yenu katika roho na nafsi zenu.

Lakini mnaweza kushinda kwa kusimama katika Neno langu ambalo ni upanga wa Roho mikononi mwenu.

Nimesema katika Yoshua 1:8 ya kuwa mtafanikiwa ikiwa mambo matatu yatafanyika juu ya Neno langu:
(a) Lisiondoke kinywani mwenu
(b) Mlitafakari wakati wote
(c) Na kudumu kulitenda

Sasa angalia mmesimamaje katika maeneo hayo matatu. Maana hizo ni mbinu za kulitumia Neno langu kama silaha ya kumshinda adui

Mkisimama katika Neno langu ninavyotaka mtavuna mafanikio sana kwa wakati wangu msipozimia na kukata tamaa katika mioyo yenu.

roho ya mpinga Kristo inawakatisha tamaa kwa kuwaangaliza matokeo ya upungufu mlionao badala ya kuangalia ahadi zangu na matokeo yake.

Kwa kadri mnavyoangalia matokeo ya upungufu mlionao, ndivyo mnavyozidi kutafakari juu ya upungufu mlionao. Kwa kadri mnavyozidi kutafakari juu ya upungufu mlionao, ndivyo mnavyozidi kukiri na kushuhudia upungufu mlionao na matokeo yake.

Kumbuka mnayafunga mafanikio yenu kwa maneno ya vinywa vyenu yanayotoka katika nafsi zisizotafakari ahadi zangu na matokeo yake.

Mimi si mtu hata niseme uongo. Nililolisema katika Neno langu nimesema nitalitimiliza. Napenda kufanikiwa kwenu kuliko nyinyi mnavyopenda kufanikiwa kwa watoto wenu. Msikubali adui ayumbishe macho yenu na mioyo yenu isione uaminifu wangu.

Mkisimama katika neno langu na kupigana hivyo vita vizuri vya imani mlivyo navyo;
- mtashangilia ushindi wakati kuta hazijaanguka bado,
- mtatangaza ushindi wakati bado upinzani wa adui umesimama,
- mtaona mafanikio wakati bado mmezungukwa na upungufu,

Kumbuka neno langu linatangaza ushindi katika roho kwanza kabla ya haujaonekana kwa nje. Ndicho kilimchomsaidia Ibrahimu wakati anasubiri mtoto wake. Na ndicho kilichonisaidia na mimi pale masalabani - nilishangilia ushindi dhidi ya adui hata kabla sijafufuka. Daudi naye aliuona ushindi wakati bado Goliati amesimama mbele yake.

Kila mtu atakuja kwangu na kuuliza nimpe Neno la kusimamia katika vita alivyo nayo. Hamuwezi kushinda pasipo Neno.

Haya ndiyo machache tuliyoyapokea kutoka kwa Bwana Yesu tulipofanya maombi ya kuuliza kwa nini watu wengi wa Mungu wamekuwa hawafanikiwi vizuri katika eneo la fedha. Ingawa Bwana alisema nasi mwaka 1997 tunaamini bado ujumbe una nguvu ndani yake ya kukusaidia. Tafakari maneno ya ujumbe huu, weka katika matendo yaliyomo - na Mungu atakusaidia!

Ahsante,

Mwl. Christopher Mwakasege

 

Shalom

Je Mungu ni sehemu ya mazungumzo yako ya kila siku na watoto wako? Au unakwepa kuongea nao habari za Mungu? Watoto wako wanamuona Mungu katika maneno yako ya kila siku? Kitu unachokithanimi utawekeza muda wako, mali na hata nguvu zako. Watoto wako waone jinsi unavyowekeza kwa Mungu katika kulisoma neno lake, kuomba, kuhudhuria kanisani na kutumika katika kazi ya Mungu.

Tunapozungumza ukuu wa Mungu na watoto wetu katika maisha ya kila siku tunawajengea hazina kubwa ya imani kwa Mungu wao ambayo watakuwa nayo siku zote. Pamoja na kuwahamasisha kupata maksi nzuri darasani, kujihusisha na michezo na kufanya kazi za nyumbani hakikisha unawafundisha kumtumikia Mungu katika umri wowote walionao. Neno la Mungu liwe sehemu ya maisha yako na watoto wako siku zote.

KumbuKumbu 11:18-19 “Kwa hiyo yawekeni maneno yangu mioyoni mwenu na rohonu mwenu; yafungeni yawe dalili juu ya mikono yenu, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yenu. Nayo yafunzeni Vijana vyenu kwa kuyazungumza uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo“

 



Chanzo: https://womenofchrist.wordpress.com

Bila ya kuwa na maono ya wapi unaelekea ni rahisi kuchukuliwa na upepo na kupelekwa usikokutazamia. Maono yatakufanya ujue ni nini ufanye kwa ajili ya Mungu na maisha yako kwa ujumla.

Mithali 29: 18 

Maono yako kwa ajili ya kazi ya Mungu ni lazima yaendane na agizo kuu alilolitoa Bwana Yesu kwa wote wanaomwamini.

Marko 16:15 Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri injili kwa kila kiumbe.

Ni lazima mara zote agizo hili liwe ndani yako ili unapoendelea na maono yako usijeenda mbali na agizo hili.

Shetani hujaribu kuyafisha maono yako na usipokuwa mwangalifu atayapoteza kabisa. Yeye mara zote hutaka kituzuia kuyafanya mapenzi ya Mungu, anajua akiyaua maono yetu hatutaweza kuifanya kazi ya Mungu kwa ukamilifu.

2Korintho 2:11 Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake.

Mambo yafuatayo shetani huyatumia kuua maono yetu:

1. Dhambi ambazo hazijatubiwa
Isaya 59:9-12 Mistari hii inaonyesha kuwa dhambi isipotubiwa hupofusha macho ya rohoni hivyo hutaweza kuyaona maono yako. Dhambi inakuweka mbali na utukufu wa Mungu.

2. Uhusiano uliovinjika katika mwili wa Kristo 
Tunaporuhusu makosa ya ndugu zetu katika Kristo kuzaa uchungu badala ya kusamehe, tunaruhusu shetani kuyafunga macho yetu ya kiroho na hivyo kushindwa kuiona njia ya kuelekea kwenye maono yetu.

3. Tamaa ya mambo yanayoonekana

Zaburi 119:37 Unigeuze macho yangu nisitazame yasiyofaa, unihuishe katika njia yako.

Ukiangalia sana mambo ya dunia na tamaa zake utajikuta unayasahau maono yako na kubaki umefungwa na mambo hayo.

4. Kuangalia sana mambo ya nyuma.

 Unapoacha kutazama mbele unapoelekea na kuweka nguvu na akili yako yote katika mambo ya nyuma yaliyopita, utapoteza kusudi lako na maono yako.

Mwanzo 19:26 Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi.

Wafilipi 3:13 Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele.

5. Kutumia muda mwingi kuangalia matatizo

Shetani hujaribu kutufanya tuangalie tu matatizo tuliyonayo na yale yanayoweza kutokea tunapoyafanyia kazi maono yetu hivyo kutuondolea imani ya kuyakamilisha. Biblia katika kitabu cha hesabu inaelezea habari za wapelelezi kumi waliorudi na habari za kukatisha tamaa katika kuiendea nchi ya ahadi maana waliangalia zaidi matatizo na kupoteza maono yao ya kuingia nchi ya ahadi.

Joshua na Kaleb waliona zaidi ya matatizo, waliuona ukuu na uaminifu wa Mungu. Hawakuwa na hofu yoyote hivyo waliweza kuingia nchi ya ahadi (kukamilisha maono yao) maana walimwamini Mungu. Petro alijaribu kutembea juu ya maji lakini alipoona mawimbi akasahau Yesu aliyekuwa mbele yake akimwambia njoo, akaweka akili kwenye mawimbi akaanza kuzama.

Ili tuweze kuyafanikisha maono yetu ni lazima tuwe na uhusiano na ushirika wa karibu na Roho Mtakatifu.

Ubarikiwe na BWANA Yesu.




 chanzo: https://womenofchrist.wordpress.com

Mambo ya nyuma yasikufanye ushindwe kuifurahia leo yako au kupanga mipango kwa ajili ya kesho yako. Hakuna ambaye hajawahi kuumizwa iwe ni maisha/ mtu / watu au hali. Kinachotofautisha ni uamuzi wa kuachilia maumivu na machungu ya nyuma na kusonga mbele. Kuendelea kuyashikilia na kuyabeba kama bango haiondoi uhalisia kuwa yametokea wala hakufanyi leo yako kuwa nzuri.

Tambua kuwa maisha yako ni jukumu lako na si mwingine yeyote. Haijalishi umeumizwa vipi, unawajibika kuishi maisha yako kwa furaha na kufanya bidii ili kesho iwe bora zaidi. Aliyekukosea au kukusababishia maumivu hawajibiki kukupa furaha wala kukuondolea maumivu, ni jukumu lako asilimia mia. Amka sasa, jikung’ute maumivu yote na uchungu wa yaliyopita na usonge mbele.

Si kwa uweza wala nguvu zetu bali kwa msaada wa Mungu.



chanzo: https://womenofchrist.wordpress.com

Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho. —YEREMIA 29:11

Iwapo una picha mbaya binafsi kujihusu, tayari imeathiri vibaya mambo yake ya kale, lakini unaweza kuponywa na kutoruhusu ya kale kujirudia. Ninakuhimiza kusahau yaliyopita hata mambo yoyote hasi ambayo umehisi kujihusu na kujisukuma mbele kuelekea vitu ambavyo Mungu amekuwekea.

Mungu ana mpango mwema na kusudi kwa kila mmoja wetu na njia maalum na wakati mtimilifu wa kuyafanya yatimie, lakini sio sisi wote tunayaona haya. Wakati mwingi tunaishi chini ya kiwango cha maisha ambayo Mungu anakusudia tufurahie.

Kwa miaka mingi sikutumia haki na faida zangu kama mwana wa Mungu. Ingawa nilikuwa Mkristo na kuamini nitaenda mbinguni nitakapofariki, sikujua kwamba kuna jambo ambalo lingefanywa kuhusu maisha yangu yaliyopita, yaliyopo na yajayo. Nilikuwa na picha mbaya kujihusu, na ikaathiri maisha yangu ya kila siku, pamoja na mwono wangu wa siku zijazo.

Leo unaweza kukubali upendo wa Mungu juu yako na uufanye upendo wake msingi wa kujipenda na kujikubali. Pokea hakikisho lake, ukijua kwamba unabadilika na kuwa vile anavyotamani uwe. Halafu uanze kujifurahisha—ulipo—ukiwa njiani kuelekea ukomavu mkamilifu wa kiroho.

Acha Mungu awe Mungu katika maisha yako. Mweke katika kiti cha dereva. Anajua analofanya.

 

Umngoje Bwana, uwe hodari, upige moyo konde, naam umngoje Bwana. —ZABURI 27:14

Tukimngoja Mungu, hatuwi wavivu au kukosa kujishughulisha, lakini kwa kweli tunajishughulisha kabisa kiroho. Huenda tusiwe “tunafanya” kitu, lakini tunamwamini Mungu kufanya yanayohitajika kufanywa. Kwa maneno mengine, tunasema, “Bwana, sitajaribu kufanya haya kwa nguvu zangu. Nitakungoja uniokoe. Na nitaendelea kufurahia maisha yangu huku nikikungoja.”

Shetani anataka tusikitike kutokana na kujaribu kutatua matatizo yetu wenyewe. Anachukia furaha yetu. Anataka kuona kitu kingine lakini si furaha, kwa sababu furaha ya Bwana ni nguvu zetu (Nehemia 8:10). Wasiwasi huiba furaha yetu, lakini furaha hututia nguvu.

Huwa tunajaribiwa kufikiri hatufanyi yanayotupasa kufanya tusipokuwa na wasiwasi au kutafuta jibu la matatizo yetu, lakini hili litazuia wokovu wetu badala ya kuusaidia. 

Si kutowajibika kufurahia maisha huku tukimngoja Mungu na kumtarajia kufanya kile tusichojua kukifanya!

Usihofu kwa kuwa vita si vyako, ni vya Bwana.


Author: Joyce Meyer
Source: https://tv.joycemeyer.org/kiswahili/devotional/kungoja-mungu/

Utangulizi

SI MAPENZI YA MUNGU TUWE MASIKINI!

(Namna ya mkristo kuishi katika hali ngumu ya uchumi bila kumkosea Mungu)

            Kati ya mambo yaliyotabiriwa kutokea katika siku hizi za mwisho ni dhiki katika mataifa, pamoja na hali ngumu ya uchumi. Soma mwenyewe katika Luka 21:25-26 na Ufunuo wa Yohana 6:5-6.

          Pia, tunasoma kutoka katika biblia ya kuwa biashara na uweza wa kuuza na kununua utafuata mfumo fulani uliojaa dhuluma, ambao utatawaliwa na kundi fulani ulimwenguni. Watu hawatauza wala kununua bila ya kupatana na watu wa kundi hilo, na hasa kiongozi wao. Na asomaye na afahamu. Soma kitabu cha Ufunuo wa Yohana sura yote ya 13.

          Si hivyo tu, bali biblia inaeleza wazi kabisa kuwa katika siku hizi za mwisho kutakuwa na uhusiano mkubwa sana kati ya utajiri na uasherati na pia kati ya biashara na uasherati. Soma kitabu cha Ufunuo wa Yohana sura za 17 na 18. Lakini pia unaweza kuwa na utajiri na ukafanya biashara bila kujihusisha na uasherati na mambo mengine yaliyo kinyume na maadili ya Mungu.

              Tutawezaje kupona katika hali ya namna hii tusimkosee Mungu wetu aliyetuita katika utakatifu ndani ya Mwana wake mpendwa Yesu Kristo? Kwa nini wakristo wengi wanaishi katika hali ngumu kiuchumi kama vile kuna mtu aliyewawekea vikwazo vya uchumi wasifanikiwe?

          Watu wengi wanapenda kuishi maisha matakatifu na wengi pia wanapenda kuokoka na kudumu ndani ya kristo, lakini swali linalowasumbua ni wafanyeje katika hali ngumu hii ya uchumi wapate chakula, malazi na mavazi kihalali bila kumkosea Mungu?

          Ni watu wachache wanaofahamu uwezo wa mawazo katika kuongoza maneno na matendo yao ya kila siku. Ni budi ufahamu ya kuwa maneno yako na matendo yako ni matokeo ya jinsi unavyowaza. Kwa maneno mengine naweza kusema ya kuwa maisha ya mtu yanategemea mtazamo wa mawazo yake.

              Kwa ufafanuzi zaidi ni kwamba jinsi ulivyo ni matokeo ya jinsi unavyowaza; kwa kuwa unayowaza ndiyo unayoyasema na kuyafanya.

          Watu wengi wamekuwa wakifikiri ya kuwa Mungu ndiye aliyewapangia kuwa maskini. Na hata wakristo wengine kudiriki hata kuuona umaskini kama sehemu ya utakatifu na unyenyekevu.

          Lakini Biblia haisemi hivyo, wala haifundishi mawazo hayo. Ni lengo langu kukueleza katika ujumbe huu ya kwamba SI MAPENZI YA MUNGU TUWE MASKINI.

           Nataka ufahamu pia ya kuwa nitakapokuwa natumia neno wakristo katika ujumbe huu, ujue namaanisha wakristo wale wanaomkiri Yesu Kristo ya kuwa Bwana na Mwokozi wao; ambao pia humwabudu Mungu katika Roho na Kweli.

          Ni maombi yangu kwa Mungu katika Jina la Yesu Kristo kuwa atakuwezesha kusoma na kuelewa somo hili, ili wote tulio wakristo tusimame katika haki zetu zote zilizopatikana pale msalabani. Nia hasa ni kukupa mafundisho ya msingi ya kukusaidia uweze kuishi hata katika hali ngumu ya uchumi bila kumkosea Mungu. Kila wiki nitakuwa nakuwekea sura mojawapo ya mafundisho haya.

Mafundisho ninayotarajia kukufundisha yatakuwa na mfululizo wa masomo kama yafuatayo:

·         Kwa nini si mapenzi ya Mungu tuwe maskini?

·         Mafundisho manne yasiyo sahihi unayopaswa kuyatambua

·         Nani anaupenda wokovu wa kimaskini?

·         Utajiri wake Kristo usiopimika

·         Uchumi wa ufalme wa mbinguni

·         Tofauti ya zaka na dhabihu

·         Ukitoa tegemea kupokea

·         Sadaka na wokovu

·         Natoa lakini sipokei – nifanyeje?

·         Ufanyeje katika hali ngumu ya uchumi?

    Haya ni mafundisho ambayo nitayaweka kwa namna ambayo yatakupa changamoto ya kuyasoma zaidi wewe binafsi na kuyaweka katika matendo. Kwa hiyo usitegemee kupata majibu ya maswali yote uliyonayo juu ya mambo niliyoorodhesha hapa juu, bali tegemea mwongozo wa changamoto itakayokusaidia katika kujifunza zaidi juu ya utajiri  na mkristo.

 

KWA NINI SI MAPENZI YA MUNGU TUWE MASKINI?

              Napenda kuanza kukuambia ya kuwa si mapenzi ya Mungu uwe maskini. Kwa sababu tangu kuwekwa misingi ya ulimwengu huu, Mungu hakupanga kuwa watu wake aliowaumba wawe maskini; bila kujali rangi, kabila, wala taifa.

                Nafahamu ya kuwa katika Mathayo 5:3, Yesu Kristo alisema; “Heri walio maskini wa roho; maana ufalme wa mbinguni ni wao.” Watu wengi wanapousoma mstari huu, wanadhani Yesu Kristo alisema “Heri walio maskini wa mahitaji ya MWILI; maana ufalme wa mbinguni ni wao.” Lakini Kristo hakusema hivyo.

              Mtu maskini maana yake ni mtu mhitaji. Yesu Kristo aliposema “Heri walio maskini wa roho …….” Alikuwa ana maana ya kusema ‘Heri walio wahitaji wa mambo ya rohoni; maana ufalme wa mbinguni ni wao. Ndiyo maana aliongeza kusema, “Heri wenye njaa na kiu ya haki; maana hao watashibishwa" (Mathayo 5:6).

          Mtu aliye maskini wa mambo ya mwili ni yule aliye mhitaji wa mambo ya mwili. Na mambo ya mwilini ninayoyasema ni mavazi, chakula na mahali pa kulala. Yesu Kristo hakusema heri wale walio na mahitaji ya chakula, mavazi, afya na malazi.

          Ninaposema mahitaji ya mwili usije ukachanganya na matendo ya mwili yaliyoandikwa katika Wagalatia 5:19-21 ambayo ni uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda na ulevi. Mimi siyazungumzii hayo ninaposema juu ya mahitaji ya mwili. Mahitaji ya mwili ninayoyasema ni mavazi, chakula, nyumba na matibabu.

          Kwa hiyo si sawa kabisa kwa mtu kuhalalisha umaskini wa mwili, yaani ukosefu wa chakula, mavazi, matibabu na nyumba, kwa kutumia maneno ya Bwana Yesu Kristo yaliyo katika Mathayo 5:3:

Nataka kurudia tena; si mapenzi ya Mungu mtu awe maskini.

          Unaweza ukaniuliza na kusema, “Bwana Mwakasege kama si mapenzi ya Mungu mtu awe maskini, mbona basi kuna matajiri na maskini, je! Mungu hakuwaumba wote?

          Ni kweli kwani hata imeandikwa katika Mithali 22:2, kuwa “Tajiri na maskini hukutana pamoja; Bwana ndiye aliyewaumba wote”. Lakini fahamu ya kuwa ingawa matajiri na maskini waliopo wote waliumbwa na Mungu; tangu mwanzo wa uumbaji Mungu hakuyaweka matabaka haya mawili.

          Hapo mwanzo Mungu alipomuumba mtu, hakuweka ndani yake utajiri na umaskini pamoja. Wala hakuumba watu wengine wawe matajiri na wengine wawe maskini.

              Tunafahamu ya kuwa mtu aliumbwa kwa mfano wa Mungu na kwa sura ya Mungu. Na naamini ya kuwa utakubaliana nami nikisema Mungu wetu si maskini kwa hiyo hatukuumbwa kwa mfano wa kimaskini wala sura ya kimaskini.

          Kwa nini nasema na kusisitiza ya kuwa si mapenzi ya Mungu tuwe maskini?

            Ninazo sababu nne ambazo ningependa kukushirikisha:

Mungu ndiye atupaye nguvu za kupata utajiri

“ Bali utamkumbuka Bwana , Mungu wako, maana ndiye akupaye NGUVU ZA KUPATA UTAJIRI; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo” (Kumb. 8:18).

          Si mapenzi ya Mungu tuwe maskini kwa kuwa yeye mwenyewe ndiye atupaye nguvu ili tupate utajiri! Kama basi Mungu anatupa nguvu za kupata utajiri, ina maana ni wazi kwamba Mungu hapendi tuwe maskini wa mambo ya mwilini.

         Lakini fahamu ya kuwa si matajiri wote waliopo duniani wameupata utajiri kutokana na nguvu walizopewa na Mungu. Wengi wamepata utajiri kwa njia ya dhuluma. Na ndiyo maana sehemu nyingi katika Biblia matajiri wa jinsi hiyo wamekemewa. Soma Amosi 5:11, 12. Kwa sababu hii Mungu hayuko upande wa matajiri hawa. Hii pia haimaanishi kuwa Mungu yuko upande wa KILA  maskini aliopo duniani. La hasha! Mungu yuko upande wa yule ayafanyaye mapenzi yake awe tajiri au maskini (Mathayo 7:21)

        Watu wengi wametajirika kwa njia ya rushwa na kutokusimamia haki pamoja na uchoyo. Na hii si sawa hata mbele za Mungu. Ni dhambi zilizo wazi kabisa. Na wote wafanyayo hayo wanahitaji kutubu!

        Ngoja nikueleze jambo muhimu: Mungu anapokupa nguvu za kupata utajiri, anakupa akiwa na lengo na kusudi muhimu.

          Ni lengo gani hilo?

          Imeandikwa, “………. Ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo”

       Na Yesu Kristo alisema, “ ……. Kikombe hiki ni AGANO JIPYA KATIKA DAMU YANGU, inayomwagika  kwa ajili yenu” (Luka 22:20).

          Mungu akikupa nguvu za kupata utajiri ni kwa ajili ya kulifanya imara agano lake katika damu ya Yesu Kristo. Na hii ina maana utajiri utakaokuwa nao kutoka kwa Mungu ni kwa kueneza injili! Ni kwa ajili ya kueneza habari njema ya ukombozi kutokana na dhambi, mauti, magonjwa na umaskini. Habari njema hii inatakiwa kuenezwa kwa maneno na kwa matendo.

        Kwa kuwa tu kuna matajiri wasio wa haki basi haimaanishi kuwa matajiri wa haki hawapo. Ni budi tuweze kutofautisha utajiri ulio wa haki na utajiri usio wa haki.

Mungu ndiye atufundishaye kupata faida

Mungu wetu tunayemwabudu na kumtumikia katika Kristo Yesu si Mungu wa hasara bali Mungu wa faida. Imeandikwa hivi;

  “ Bwana, Mkombozi wako, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi;Mimi ni Bwana, Mungu wako,   nikufundishaye  ili upate faida, nikuongozaye katika njia  ikupasayo kuifuata” (Isaya 48:17).

           Ndiyo maana kila mtu ndani yake ameumbiwa kupenda kufundishwa ili apate faida katika mambo anayoyafanya. Mungu akikufundisha kupata faida; njia utakayotumia kupata faida itakuwa njia ya haki. Na faida hiyo haitakuwa kwa ajili yako mwenyewe, bali utawashirikisha na wengine pia faida hiyo .

          Watu wengine kwa kutokuwa wavumilivu, na kutokujali mafundisho ya Mungu; wameamua kujipatia faida kwa kuwadhulumu, kuwakandamiza na kuwanyonya wengine. Na inasikitisha jinsi wanavyomshirikisha Mungu katika faida najisi namna hiyo waposema ya kuwa ni Mungu aliyewasaidia ‘kudhulumu na kunyonya’. Ni wazi ya kuwa Mungu hakuwasaidia kupata faida kwa njia ya udhalimu.

        Si mapenzi ya Mungu tuwe maskini, ndiyo maana anatufundisha ili tupate faida ya halali. Kwa ajili hiyo imeandikwa; “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji” (Waefeso 4:28).

        Je! Si jambo la kushukuru hili, la kuwa na Mungu ambaye hapendi tupate hasara?

       Kama Mungu asingekuwa anapenda tufanikiwe katika mahitaji yetu ya mwili, basi ingeandikwa wazi katika Biblia. Lakini badala yake naona maneno kama yafuatavyo; “Mpenzi, naomba ufanikiwe katika mambo YOTE na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo” (3Yohana 1:2).

       Kwa maneno mengine anatuombea ya kuwa kwa kadri roho inavyofanikiwa basi tufanikiwe vivyo hivyo katika mahitaji ya mwili – yaani tuwe na chakula, mavazi, n.k.

Vitu vyote vyema ni mali ya Bwana, na vyote vya Bwana ni vyetu ndani ya Kristo

              Katika Zaburi 24:1 imeandikwa;“Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana; Dunia na wote wakaao ndani yake”

            Na pia ukisoma katika Hagai 2:8 unaona imeandikwa hivi “Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu, asema Bwana wa majeshi”

          Ngoja nikuulize swali; Je! unadhani vitu vyote hivi Bwana amemwekea nani? Unadhani alimwekea shetani na watu wanyonyaji wachache?

La hasha!
        Mungu aliviweka vitu hvi vyote na mali hii yote kwa ajili ya watu wake wote, ili itumike katika usawa. Kwa nini? Kwa kuwa Mungu hapendi watu wake wawe maskini. Ndiyo maana mtu alipoumbwa aliwekwa awe wakili wa mali yote ya Mungu hapa duniani.

        Utajiri uliomo duniani umetawaliwa na watu wachache na nchi chache siku hizi kwa sababu ya dhambi za uchoyo, ubinafsi, uonevu,unyonyaji, unyang’anyi na dhuluma zilizoingia ndani ya mwanadamu.
         
Na hii imefanya watu wengine kufikiri ya kuwa Mungu ndiye aliyegawa matabaka haya mawili, ambavyo si kweli. Na si vizuri kumsingizia Mungu katika jambo ambalo mwanadamu mwenyewe amejiletea uharibufu.

Yesu Kristo alikuwa maskini ili sisi tuwe matajiri

              “ Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi   alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake” (2 Wakorintho 8:9).          

            Je! unafahamu kwa nini Yesu Kristo aliamua kuwa maskini? Ni “…….. ili kwamba ninyi mpate kuwa MATAJIRI kwa umaskini wake”.

           Najua kuna wengine watashangaa kuusoma mstari huu; lakini ndivyo ilivyo.

          Nimewahi kusikia mkristo mmoja akisema: “ Mimi ni maskini kwa kuwa Yesu Kristo alikuwa maskini”.

          Na mwingine alisema; “ Napenda kuwa maskini kwa kuwa Yesu Kristo alikuwa maskini”.

         Nadhani kuwa kuna wakristo wengi ambao wana mawazo kama haya. Ni kweli kwamba Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani alikuwa maskini. Lakini hakuwa maskini ili sisi tuwe maskini; bali alikuwa maskini ili sisi tuwe matajiri! Kama alikuwa maskini ili sisi tuwe maskini kama wengine wanavyodhani, basi kazi hiyo haina faida kwetu. Lakini Yesu Kristo asifiwe kwa kuwa alikuwa maskini ili sisi tuwe MATAJIRI.

        Na ndiyo maana alisema katika Luka 4:18a ya kuwa; “Roho wa Bwana yu juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri MASKINI habari njema.”

        Je! kuna habari njema kwa maskini zaidi ya kumwondoa katika umaskini wake?

       Injili ni habari njema. Na injili ni uweza wa Mungu uuletao wokovu kwa kila aaminiye (Warumi 1:16). Kuokoka si kuenda tu mbinguni; bali kuokoka maana yake ni uokolewe usiende motoni bali uende mbinguni ukifa, PAMOJA na kuokolewa kutoka kwenye  matatizo ukiwa hapa duniani ambayo ni pamoja na umaskini.

       Petro aliposema “Bwana niokoe” alipokuwa anazama katika maji unafikiri alikuwa anataka wakati huo aokoke aende mbinguni? La hasha! Yeye Petro alitaka aokoke ASIZAME KATIKA MAJI. Na Yesu akasikia kilio chake akamwokoa. Hivi leo kuna watu wengi mijini na vijijini wanalia Yesu awaokoe kutokana na njaa, kukosa mavazi, magonjwa, maonezi, nakadhalika. Kanisa kama mwili wa Kristo linatakiwa kuwa mstari wa mbele kuwasaidia watu hao, kwa kuwa kazi hii ni sehemu ya utume wake.

       Wakristo wengine utawasikia wakisema; hapa duniani hawahitaji kitu bali thawabu yao wataipata mbinguni. Lakini matamshi ya namna hii yanaeleza ukweli nusu na usiokamilika. Kuwa mkristo kuna thawabu duniani na kuna thawabu mbinguni.

       Kama hakuna thawabu yoyote tunayoipata tukiwa hapa duniani kwa kumfuata Yesu Kristo; basi ukristo wetu hauna maana na hauna msaada wowote kwa mwanadamu. Ukristo usiotatua matatizo ya mwanadamu ya kila siku, ni ukristo usio na uhai.

        Mtume Petro naye aliwahi kusumbuliwa sana na jambo hili, hata ikabidi amuulize Bwana Yesu.

        “Ndipo Petro akajibu, akamwambia, tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata, TUTAPATA NINI BASI?” (Mathayo 19:27)

          “Yesu akasema, Amini, nawaambiaeni, hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa MARA MIA SASA WAKATI HUU, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele” (Marko 10:29,30).

          Majibu haya ya Bwana Yesu, yanazidi kutudhihirishia ya kwamba si mapenzi ya Mungu tuwe maskini. Yesu Kristo ameeleza wazi kabisa ya kuwa atakayemwamini na kufuata maagizo hayo atapata MARA MIA SASA WAKATI HUU akiwa bado duniani. Na kati ya vitu atakavyopewa ni pamoja na nyumba na mashamba!

          Ni kweli Bwana Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani alikuwa maskini, lakini baada ya kufufuka alirudishiwa utajiri wake. Ndiyo maana Mtume Paulo anazungumzia juu ya “….. utajiri wake Kristo usiopimika”. (Waefeso 3:8). Na katika Wafilipi 4:19 tunasoma hivi; “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu”.

          Kumbuka ya kuwa; Yesu Kristo alichukua dhambi zetu na magonjwa yetu , na kwa kupigwa kwake sisi tumepona (Isaya 53:5; Mathayo 8:16,17; 1Petro 2:24). Na kwa kujua hili kanisa linajihusisha na kuombea wagonjwa na kutoa huduma za afya kwa wagonjwa.

        Kumbuka ya kuwa; Yesu Kristo alichukua dhambi zetu na akafanyika dhambi kwa ajili yetu, “ Ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye” (2Wakorintho 5:21). Na kwa kujua hili kanisa linahubiri habari za ondoleo la dhambi kwa yeyote atakayemwamini Kristo.

        Kumbuka ya kuwa; Yesu Kristo alikuwa maskini, ingawa alikuwa tajiri, ili kwa umaskini wake sisi tupate kuwa matajiri (2 Wakorintho 8:9). Na kwa kujua hili kanisa linajihusisha na miradi mbalimbali ya kimaendeleo ili mtu aondokane na umaskini.

MAMBO MANNE UNAYOPASWA KUYAJUA

            Kuna mafundisho ambayo si sahihi yaliyowafanya wakristo wengi hasa wale waliookoka kutokujua cha kuamini juu ya uhusiano wa ukristo wao na utajiri. Na tuangalie maeneo manne yafuatayo ambayo wakati mwingine yamezaa mafundisho yasiyo sahihi:

TAJIRI NA UFALME WA MUNGU:

            Nadhani utakuwa umewahi kusikia watu wakisema; “Matajiri hawataurithi ufalme wa Mungu” Na wanasema ndivyo Bwana Yesu alivyosema baada ya tajiri aliyetaka uzima wa milele kukataa kuuza mali yake.

            Hata mimi mwanzoni ilikuwa karibu sana nikubaliane na usemi huu. Lakini baada ya kuyachunguza maandiko niliona ya kuwa Yesu Kristo hakusema hivyo bali anasingiziwa tu.

            Yesu Kristo alisema hivi;“Kwa shida gani wenye mali WATAUINGIA ufalme wa Mungu” (Luka 18:24)

Kwa mstari huu tunajua ya kuwa Yesu Kristo hakusema ya kuwa wenye mali hawatauingia ufalme wa Mungu; bali alisema “kwa shida gani wenye mali watauingia ufalme wa Mungu!”

            Na akaendelea kusema, “ Kwa maana ni vyepesi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Luka 18:25). Na wale waliosikia wakashtuka na kushangaa, kwa maana waliona itakuwa vigumu sana kwa tajiri kuokoka, na naona walifikia mawazo kama waliyonayo wengi siku hizi ya kuwa tajiri hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu. Ndiyo maana wakauliza “Ni nani basi awezaye kuokoka?” (Luka 18:26).

Yesu Kristo akawajibu akasema;“Yasiyowezekana kwa wanadamu yawezekana kwa Mungu” (Luka 18:26).

Kwa maneno mengine alikuwa anasema tajiri anaweza KUWEZESHWA NA MUNGU kuingia katika ufalme wa Mungu akiiamini injili inayookoa. Hata hivyo maskini naye anaokolewa kwa neema ya Mungu.

Na kwa kuamini kuwa tajiri hawezi kuurithi ufalme wa Mungu, wakristo wengi kwa kudhamiria kabisa wameamua kuwa maskini ili wasije wakaukosa ufalme wa Mungu. Lakini hii si sawa na ni kukwepa wajibu wetu tulionao kama mawakili wa mali zote za Mungu.

            Na ni vizuri ufahamu ya kuwa umaskini wa kukosa chakula, mavazi na nyumba ya kukaa siyo tiketi ya kuingia katika ufalme wa Mungu. Na wala umaskini siyo utakatifu – ingawa kuna maskini walio watakatifu! Na pia utajiri siyo utakatifu ingawa kuna matajiri walio watakatifu.

            Kuna Mkristo mmoja wa dhehebu fulani alikuwa akinieleza hali iliyowasonga katika dhehebu lao; alisema;

“Katika kanisa letu Mchungaji akionekana amevaa vizuri,   wakristo wake wanasema amepoa kiroho. Kwao mtu wa kiroho  ni mtu aliye maskini, asiyevaa nguo nzuri wala viatu vizuri.”

Niliposikia maneno hayo nilisikitika sana, na nikakumbuka maneno ya Mungu aliyosema kwa kutumia kinywa cha nabii Hosea, yasemayo, “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa ….” (Hosea 4:6) na pia Yesu Kristo  aliwahi kusema ya kuwa watu wanapotea kwa kuwa hawajui maandiko wala uwezo wa Mungu.

Kwa hiyo fungua moyo wako uisikie kweli ambayo ndiyo neno la Mungu. Na utaifahamu kweli na hiyo kweli itakuweka huru (Yohana 8:32)

MUNGU NA MALI

            Kuna uhusiano gani kati ya Mungu na Mali? Kuna uhusiano gani kati ya Mkristo na Mali? Kuna uhusiano gani kati ya wokovu na mali?
Je, ni dhambi kwa mkristo kuwa na mali nyingi? Hebu na tuangalie maneno ya Yesu Kristo juu ya Mungu na Mali.

            “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili, Kwa maana  atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu  na Mali” (Mathayo 6:24)

Neno la kiingereza lililotafsiriwa na kuandikwa ‘mali’ ni ‘mammon’ Na neno hili ‘mommon’ ni jina la roho ya ibilisi inayotawala mali. Kwa maneno mengine naweza kusema kuwa ‘mammon’ ni jina la pepo.

            Kwa hiyo, neno ‘mali’ lilivyotumika hapa linamaanisha ‘pepo linaloitwa Mali’ Ndiyo maana Yesu Kristo alisema; “Hakuna  mtu awezaye kutumikia MABWANA wawili ….” Yesu Kristo asingeliita mali kuwa ni mojawapo ya MABWANA kama hakuwa anasema juu ya roho inayoitwa mali. Roho hii ya shetani iitwayo Mali imewafanya watu wengi, hata wakristo waache kumtumikia Mungu aliye hai, na badala yake waitumikie roho inayowasukuma na kuwatamanisha juu ya mali, ili waitumie kwa uchoyo na ubinafsi.
            Wakristo wengine wanadhani wanaweza kumtumikia Mungu na vile vile wamtumikie Mali. Yesu Kristo alisema; “HAKUNA mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana ATAMCHUKIA HUYU, NA KUMPENDA HUYU: AMA ATASHIKAMANA NA HUYU, NA KUMDHARAU HUYU. Hamwezi kumtumikia Mungu na Mali.”

Kwa kusema hivi hakuwa anamaanisha kuwa na vitu vinavyoitwa mali ni vibaya. Kitu anachosema ni kibaya ni KUITUMIKIA MALI! Biblia inasema katika Zaburi 24:1 kuwa, “Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana; Dunia na wate wakaao ndani yake.”

Mtu hakuumbwa ili kuitumikia mali. Mtu aliumbwa kwa ajili ya utukufu wa Mungu na amtumikie Yeye peke yake. Mali ya dunia iliwekwa kwa ajili ya kumtumikia mtu, na siyo mtu kuitumikia mali! Mtu aliwekwa juu ya mali yote na aliagizwa kuitawala (Mwanzo 1:28 – 30).

Kuwa na mali siyo vibaya, wala siyo dhambi. Mali inakuwa kikwazo katika maisha ya ukristo inapoanza kumfanya mtu amsahau Mungu na mapenzi yake. Ndiyo maana Yesu Kristo alisema; “Kwa shida gani wenye mali watauingia ufalme wa Mungu” (Luka 18:24) siyo kwamba hawezi kuuingia ufalme wa Mungu, bali kwa shida wenye mali watauingia ufalme wa Mungu. Kwa maneno mengine ni kwamba wakimtanguliza na kumtumikia Mungu, mali haitakuwa kwazo katika maisha yao ya ukristo.

Sasa tuishije katika ushauri wa namna hii?

            “Kwa sababu hiyo  nawaambieni, msisumbukie maisha   yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? NI YUPI KWENU AMBAYE AKIJISUMBUA AWEZA KUJIONGEZA KIMO CHAKE HATA MKONO MMOJA? Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini  maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti; nami nawaambia ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, JE! HATAZIDI SANA KUWAVIKA NINYI, ENYI WA IMANI HABA? Msisumbuke basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote” (Mathayo 6:25 – 32)

            Kuna wakristo wengine wameyaelewa vibaya maneno haya ya Bwana Yesu Kristo hata kufikia kutokufanya kazi kwa kisingizio cha kwamba Yesu Kristo alisema tusiyasumbukie maisha. Kwao kufanya kazi ina maana kusumbukia maisha. Lakini napenda kukuambia ya kuwa Yesu Kristo hakuwa ana maana ya kutuambia tusifanye kazi aliposema tusiyasumbukie maisha.

Nadhani unaamini ya kuwa ni Roho wa Kristo aliyemwongoza Mtume Paulo kuwaandikia Wathesalonike juu ya mashauri mbali mbali ya kikristo. Katika 1Wathesalonike 3:10b anasema, “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.” Ni muhimu kufanya kazi. Kufanya kazi siyo kusumbuka na maisha. Kusumbuka na maisha siyo kufanya kazi.

Jambo ambalo Bwana Yesu Kristo alitaka tufahamu wakati alipokuwa akisema tusisumbukie maisha, ni kwamba katika kila jambo tumshirikishe Mungu na kumtanguliza Yeye. Wakristo wengine wanadhani wanaweza kula, kunywa na kuvaa bila msaada wa Mungu. Yesu Kristo alisema katika Yohana 15:5b kuwa; “…… maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya NENO LO LOTE” (Hili ni pamoja na kula, kunywa na kuvaa) Ndiyo maana katika Wafilipi 4:13 imeandikwa kuwa “Nayaweza mambo yote katika YEYE anitiaye nguvu” Yesu Kristo ndiye atutuaye nguvu.

Yesu Kristo alitoa mwongozo mzuri sana wa jinsi ya kuishi hapa ulimwenguni aliposema;

“Bali utafuteni KWANZA ufalme wake, na haki yake; na hayo  yote  mtazidishiwa” (Mathayo 6:33)

Ukiyaangalia maisha ya watu wengi waliookoka utadhani Yesu Kristo alisema, “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote MTAONDOLEWA.” Inahuzunisha kuona ya kuwa watu wengi wakiokoka maisha yao yanageuka kuwa duni, wanashindwa kula vizuri, wala kuvaa vizuri.

            Ngoja nirudie kusema kuwa SI MAPENZI YA MUNGU TUWE MASKINI. SI MAPENZI YA MUNGU TUKOSE CHAKULA WALA MAVAZI. Ni Mungu yupi ambaye atawapenda ndege akawavika na kuwalisha, na akawaacha watoto wake aliowaumba kwa mfano wake wakose chakula na mavazi?

            Mungu wetu tunayemwabudu na kumtumikia katika Kristo Yesu, anapenda tuishi maisha mazuri, tule, tunywe na kuvaa vizuri. Tunachotakiwa kufanya ni kuutafuta KWANZA ufalme wake, na haki yake, na hayo yote (chakula na mavazi) TUTAZIDISHIWA na siyo TUTAONDOLEWA.

    Ukiona mtu anasema ameokoka na halafu anajikuta anakosa chakula na mavazi huku anafanya kazi, basi ujue anafanya kazi na kukusanya vitu hivyo pasipo Bwana; kwa kuwa asiyekusanya pamoja na Bwana hutapanya.

FEDHA NA KUPENDA FEDHA

            Nimewahi kumsikia mhubiri mmoja akisema; “Fedha ni shina la maovu, kwa hiyo wakristo wajihadhari nazo.” Na wakristo wengi wamekuwa wakisikika wakisema hivyo, kwa hiyo wanaogopa kuwa na fedha za kutosha.

Lakini ninaposikia watu wakisema hivi, huwa najiuliza wanaupata wapi usemi huu? Biblia haisemi; “Fedha ni shina la maovu.”

Badala yake Biblia inasema hivi;“ Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha;ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi”(1Timotheo 6:10)

Kupenda fedha ni kuwa na tamaa ya fedha; ni kuzitamani fedha. Na kupenda fedha huku ndiko shina moja la mabaya ya kila namna.

Kuwa na fedha nyingi au kidogo siyo dhambi, kwa kuwa fedha ni mali ya Mungu (Hagai 2:8) Lakini kupenda fedha nyingi au kidogo ni shina moja la maovu.

Tamaa ya fedha ndiyo inayoleta wizi, ujambazi, mauaji, dhuluma, kutokutosheka, uchoyo, wivu, uasherati; nakadhalika. Lakini unaweza kuwa na fedha bila ya kufungwa na roho ya kupenda fedha.

Je! Unafahamu ni kwa nini shetani hapendi wakristo safi wawe na fedha? Maana ni kazi ya shetani kuwapiga vita wakristo wanaotaka kujipatia fedha kwa njia ya halali. Akishindwa kuwazuia kupata fedha; atahakikisha zile fedha walizonazo wanazimaliza haraka hata kwa matumizi ambayo hawakupanga.

Je! Unafahamu ni kwa nini?

Kwa sababu anafahamu mkristo safi akiwa na fedha za kutosha, atazitumia hizo kumpiga nazo vita kwa kuihubiri injili! Na shetani anafahamu kuwa Yesu alisema mwisho hautakuja mpaka injili ihubiriwe katika mataifa yote. Kwa hiyo anajua akiweza kuwakosesha wakristo fedha za kutosha ili injili ihubiriwe, yeye anapata muda wa kupumua na kupumzika.

Wengi wameshindwa kujenga makanisa kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Watumishi wa kanisa wanalipwa mishahara kidogo, kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Mikutano ya injili na semina za neno la Mungu hazifanyiki mara kwa mara kwa kukosa fedha. Wainjilisti wanatafuta fedha za kununulia vipaza sauti wanakosa. Na matokeo yake ni kazi ya Mungu kupoa.

Je! Unadhani ni nani ambaye anaweza kutoa fedha yake ili ikahubiri injili kama siyo wakristo wenyewe? Na wakristo watatoaje fedha kama hawana fedha? Na watakuwaje na fedha, kama wanadhani kuwa na fedha nyingi ni dhambi?

Na shetani ameutumia mwanya huu kuzitumia fedha ambazo wanazo watu wasiopenda haki kueneza dhambi na uovu. Je, ni haki kwa nchi nyingine kutumia ma-billioni ya fedha kutengeza silaha ambazo baadaye wanaziharibu tena, huku mamillioni ya watu wanakufa kwa njaa na maafa mengine?

        Kwa hiyo usikubali unaposikia mtu akisema kuwa na fedha ni vibaya; lakini uwe mtu wa kutokupenda fedha. Kwa kuwa ukizitamani fedha utajikuta unaanza kuzitafuta hata kwa njia ambazo ni kinyume cha maadili yetu ya Kikristo; na pia kinyume cha utu wa mwanadamu.

MASKINI NA TAJIRI

            Nafahamu ya kuwa si mpango wa Mungu kwa mtu aliye tajiri kumtawala maskini kwa sababu ya umaskini wake. Na pia nafahamu si mpango wa Mungu kwa nchi zilizo tajiri kuzitawala nchi maskini kwa sababu ya umaskini wake.

    Lakini ni vizuri tufahamu uhusiano uliopo kati ya matabaka haya mawili:-

    Biblia inasema;“Tajiri humtawala maskini, Naye akopaye ni mtumwa wake  akopeshaye.” (Mithali 22:7)

Maneno haya ni kweli kabisa, na mtu ye yote ambaye ni msomaji wa historia na magazeti, anafahamu majadiliano ya muda mrefu yaliyopo kati ya nchi tajiri na nchi maskini duniani.

Ukoloni mbaya uliopo sasa hivi kati ya nchi na nchi, ni ukoloni wa kiuchumi. Katika ukoloni huu wa kiuchumi nchi tajiri zinatumia utajiri wake katika kuzikandamiza nchi maskini. Na kwa njia hii mamillioni ya watu wamo katika hali mbaya sana kimaisha.

Na njia kuu ambayo nchi hizi tajiri zinatumia kuzitawala nchi maskini ni kwa njia ya kuzipa mikopo. Na nchi maskini zote zimejikuta zimeingia katika utummwa mbaya kwa sababu ya mikopo ambayo haijajulikana kama inaweza kulipwa yote.

Inakisiwa ya kuwa jumla ya madeni yote ya nchi zinazoendelea ni mabilioni ya dola za Kimarekani na yanazidi kuongezeka.

Ni kweli kabisa kwamba utajiri huu wa nchi hizo si wote uliopatikana kwa njia ya halali. Na wafuatiliaji wa mambo ya uchumi duniani, wanafahamu jinsi nchi hizi zilizoendelea zinavyobuni mbinu mbalimbali kuzinyonya nchi zinazoendelea.

Ingawa si mapenzi ya Mungu tuwe maskini, lakini pia si mapenzi ya Mungu tuwe matajiri ili kuwatawala wengine kwa sababu ya umaskini wao. Ole ni kwa matajiri wanaoutumia utajiri wao kuonea na kuwafanya wenzao kuwa watumwa.

Mungu anapotupa nguvu za kupata utajiri ndani ya Kristo ni kwa kusudi muhimu la kuimarisha agano lake la kumhudumia mtu mzima – kiroho na kimwili.

          Ni kweli maskini ana shida, maana hata biblia inasema maneno yake hayasikilizwi (Mhubiri 9:16). Na hii imejionyesha wazi sana katika maoni na malalamiko ya nchi maskini ambayo yanapuuzwa na kutosikilizwa na nchi tajiri.

          Lakini hali hii si kwa nchi tu, bali hata katikati yetu humu humu makanisani. Sehemu nyingi kuna wakristo ambao ni matajiri, na mara kwa mara huwa wanatumia utajiri wao katika kuwatawala viongozi wa kanisa; na hata wakati mwingine kudiriki hata kutaka kubadilisha maamuzi ya vikao vya kanisa.

          Na kwa upande mwingine viongozi wa sharika wanajikuta wameingiwa na hofu na kushindwa kuwakemea matajiri hao wakati wanapokwenda kinyume na maadili ya kikristo. Kama siyo ukoloni wa namna yake ulioingia katika kanisa ni nini basi?

          Naamini ya kuwa wachungaji na viongozi, wengi wao wangekuwa na hali nzuri kiuchumi, baadhi ya matajiri wanaotaka kutawala viongozi wengine wangeshindwa katika mbinu zao. Au wewe unasemaje?

          Shetani amekuwa akijitahidi sana kuwakandamiza wakristo wasiwe matajiri kwa kutumia njia mbali mbali kwa kutegemea mazingira yalivyo. Mahali pengine ametumia mifumo na vyombo vya fedha kama mabenki; pengine ametumia serikali, pengine ametumia mafundisho mabaya kwa wakristo, nakadhalika.

Na shabaha yake ya kufanya hivyo ni:-

(a)               Maneno ya wakristo yasisikilizwe wanapohubiri, kwa kuwa imeaandikwa; “….Walakini hekima ya maskini hudharauliwa wala maneno yake hayasikilizwi” (Mhubiri 9:19b). Kwa lugha nyingine maana yake “hayatiliwi maanani.”

(b)               Wakristo waendelee kuwa watumwa ingawa wanadai ya kuwa wamewekwa huru. Kumbuka imeandikwa hivi; “Tajiri humtawala maskini. Naye akopaye ni mtumwa wake akopeshaye” (Mithali 22;7)

        Na maneno haya ni kweli kabisa. Hebu nieleze ni nani atakayesikiliza na kuyaamini maneno ya mchungaji au mwinjilisti au mtumishi yoyote wa Mungu anayesema mtegemee Yesu katika kila kitu wakati yeye mwenyewe ana nguo yenye viraka! Jambo la kwanza ambalo msikilizaji atajiuliza ni kwamba kama huyu Yesu ameshindwa kumpa mtumishi wake nguo nzuri, atawezaje kunisaidia mimi mkristo wa kawaida?

     Kwa hiyo lazima tuwe waangalifu ili tunayosema yawe sawa na tunavyoishi. Na tuishi sawa sawa na ahadi za Mungu tunazozisimamia.

     Siku moja nilimsikia mchungaji mmoja mwanafunzi wa chuo kimoja cha biblia akisema hivi; “Kuna mtu mmoja alikuja kutufundisha kuwa sisi kama wachungaji tusisikitike tunapoona hatuna nguo nzuri, wala chakula kizuri, wala sabuni nzuri za kuogea kwa sababu IKO SIKU MOJA VITU HIVI TUTAVITAWALA NA BWANA MBINGUNI”.

     Mara moja nikamkatisha na nikasema; “ Hayo mafundisho si sawa. Unadhani Mungu aliweka hivi vitu duniani (chakula, mavazi, sabuni) kwa ajili ya shetani na watu wake? Unadhani mbinguni tukifika tutahitaji tena chakula, mavazi na sabuni? Hivi vitu Mungu aliviweka kwa ajili yetu tuvitumie wakati huu.”

 

 

NANI ANAUPENDA WOKOVU WA KIMASIKINI?

            “Nani anaupenda wokovu wa Ukristo wa kimaskini?” Ukiona mtu amefika hali ya kujiuliza swali la jinsi hii, ujue ana hali ngumu sana kiuchumi.

            Hili swali nilijikuta najiuliza mwenyewe baada ya kuwa na hali ngumu sana kimaisha baada kuokoka. Kuna wakati fulani baada ya kuokoka mimi na mke wangu tulijikuta tumefika mahali pa kukosa hata dawa ya mswaki, nguo, viatu, na chakula kizuri. Licha ya shida hizi zote bado zilifuata zingine baada ya ndugu zetu wawili tuliokuwa tunawalipia masomo yao kufukuzwa na kurudi nyumbani kwa kukosa ada. Na waliambiwa wasirudi shuleni bila nusu ya ada!

            Unadhani tulikuwa na furaha tena? Ingawa tulikuwa tunasema tumeokoka, na mtu akituambia ‘Bwana asifiwe’ tuliitika ‘Amina’ ndani ya mioyo yetu tulikuwa na vita vikali na maswali mengi.

            Ni vigumu kuieleza hali hiyo tuliyoipitia ilivyokuwa ngumu kwa maneno. Lakini utaelewa mtu mwenye familia anavyojisikia anapoona anakosa hata fedha za kuwanunulia mke na watoto wake chakula licha ya mavazi. Wakati huo tulikuwa na mtoto mmoja.

            Hali ilivyozidi kuwa ngumu, ndivyo nilivyozidi kusongwa na mawazo. Ilifika wakati ambapo nilikuwa naona aibu hata kukaa sebuleni, maana niliogopa hata kuwaangalia wale vijana waliofukuzwa shule, nikijua kuwa wataniangalia kwa macho ya huruma ili niwape ada warudi shule. Lakini si kwamba nilikuwa siwahurumii, bali sikuwa na fedha za kuwapa.

            Ningeanzaje kuwaambia kuwa sina fedha, wakati wanajua nafanya kazi, na pia waliona nilikuwa na fedha nyingi kabla sijaokoka? Jambo hili lilinifanya niwaze sana. Inakuwaje kabla sijaokoka nilikuwa na fedha nyingi na baada ya kuokoka najikuta nimefilisika? Ingawa ni kweli kwamba kabla ya kuokoka fedha zingine nilizipata kwa njia zilizo kinyume cha ukristo lakini nilikuwa nazo. Na baada ya kuokoka ilibidi niziache njia hizo – na matokeo yake nilijikuta nimefilisika.

            Lakini nilikuwa nimesoma katika Hagai 2:8 kuwa fedha na dhahabu ni mali ya Mungu. Na pia nilijua kuwa vyote vya Mungu ni vyangu nikiwa ndani ya Kristo. Kwa hiyo ilikuwa vigumu kuelewa kwa nini Mungu aseme fedha ni mali yake, halafu mimi niliye mtoto wake nisiwe nazo.

            Ningewezaje kusema wokovu ni mzuri wakati baada ya kuokoka nimejikuta sina fedha za kutosha kununua chakula, nguo, dawa ya mswaki na hata kukosa ada za watoto! Je ndivyo Mungu anavyotaka tuwe baada ya kuokoka?

            Wakati huo ndipo nilipoelewa kwa nini wana wa Israeli waliyakumbuka masufuria ya nyama ya Misri, ingawa walikula nyama hizo wakiwa utumwani. Ni rahisi sana mtu aliyeokoka kurudia njia au maisha mabaya ya kutafuta fedha kwa njia zilizo kinyume cha ukristo anapokuta anabanwa na matatizo ya kiuchumi maishani mwake. Na hata wakati mwingine unakesha katika maombi ili kumlilia Mungu akupe chakula na mavazi unaona kama vile hasikii.

            Nilipokuwa nasumbuliwa na hali hii ndipo nilipojikuta najiuliza mwenyewe; “ Nani anaupenda wokovu wa kimaskini?” Nilijikuta siupendi kabisa. Ni wokovu gani huu ambao haunisaidii hata kutunza familia yangu?

            Siku moja nilimuuliza mke wangu; nikasema; “Je! wewe unaupenda wokovu wa kimaskini?”

            Akajibu; “Hapa, siupendi!”

            Nikasema; “Naona tuna mawazo yanayofanana. Kwa hiyo naona ni muhimu tumuulize Mungu katika maombi kwa nini tulipokuwa kwa shetani tulikuwa na fedha za kutosha, lakini baada ya kuokoka na kuja kwake tunajikuta hatuna fedha hata za kununulia vitu muhimu?”

            Baada ya kukubaliana hayo, mimi na mke wangu tulianza kumwomba Mungu kwa mfululizo wa siku tatu juu ya jambo moja hilo hilo. Namshukuru Mungu kwa kunipa mke ambaye aliweza kusimama pamoja nami katika maombi juu ya jambo hili. Sijui ningekuwa na hali gani kama angelalamika. Namshukuru Mungu mke wangu hakulalamika bali ALIOMBA PAMOJA NAMI.

            Mungu alitujibu maombi na akaanza kutufundisha mambo mengi ambayo mengine nawashirikisha katika ujumbe huu.

            Tulijua hakika kuwa hayakuwa MAPENZI YA MUNGU tuwe na hali ngumu ya kimaisha namna hiyo – kukosa fedha za kutosha kununulia nguo, chakula na vitu vingine muhimu. Na baada ya kuyaweka katika matendo yale tuliyoambiwa na Bwana yaliyo katika neno lake, hali yetu ilibadilika. Na matatizo tuliyokuwa nayo wakati ule yakaisha. Tukaanza kuona furaha tena katika maisha haya ya wokovu.

            Ni vizuri kujua kuwa Mungu wetu hapendi tuwe maskini. Wala hapendi wokovu wa kimaskini! Ndiyo maana alimtuma Mwana wake wa Pekee, Yesu Kristo kutukomboa.

            Kwa kukumbusha tu, Yesu Kristo aliyafanya yafuatayo kwa kufa na kufufuka kwake:

            "Yesu Kristo alifanyika dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tuhesabiwe haki bure ndani yake ya kusimama tena mbele ya Mungu" 
(2Wakorintho 5:21)

            "Yesu Kristo aliuchukua udhaifu wetu, ili katika mambo yote tuzitegemee nguvu zake" (Mathayo 8:17; Wafilipi 4:13)
            Yesu Kristo aliyachukua magonjwa yetu, ili tusitawaliwe na magonjwa tena na kwa kupigwa kwake tumepona (Isaya 53:4,5; Mathayo 8:17; 1 Petro 2:24)
Yesu Kristo aliyachukua masikitiko na huzuni zetu, ili tukae katika amani yake ipitayo fahamu zote (Isaya 53:34; Wafilipi 4:6,7)
            Yesu Kristo alikuwa maskini kwa ajili yetu ingawa alikuwa tajiri, ili sisi tupate kuwa matajiri katika Yeye (2 Wakorintho 8:9)

Ndiyo maana matunga Zaburi 23 aliandika hivi:

“Bwana ndiye mchungaji wangu, SITAPUNGUKIWA NA KITU.Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, kando ya maji ya utulivu huniongoza. Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza katika njia za haki kwa ajili ya jina lake …. Hakika WEMA
NA FADHILI zitanifuata siku zote za maisha yangu; nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele”.

            Ni rahisi sana kusema. “Bwana ndiye mchungaji wangu, SITAPUNGUKIWA NA KITU, lakini je! Ni kweli hujapungukiwa na kitu? Je! Zaburi hii ni ya kweli, au ni maneno mazuri tu ya kutungia nyimbo?

            Lakini napenda kukutia moyo kuwa maneno haya ni ya kweli, ukikaa ndani ya Kristo hutapungukiwa na kitu. Ndiyo maana Mungu alimwambia Yoshua ya kuwa atii maagizo yake yote na kuyafanya HATAMPUNGUKIA WALA KUMUACHA (Yoshua 1:5)

            Kwa kuwa maneno haya ni ya kweli, mbona basi wakristo wengi WAMEPUNGUKIWA NA VITU? Tatizo haliko kwa Mungu, bali kwetu sisi. Na tuwe watendaji wa neno na tutaona mafanikio.


WAJIBU WA WAKRISTO:
            Ni wajibu wa wakristo (a) kusaidiana sisi wenyewe kiuchumi; na (b) Kuwasaidia kiuchumi watu wengine wasio wakristo. Kuna wakati fulani mtu mmoja alikuja kwangu kuomba ushauri.

            Nikamuuliza. “Una tatizo gani linalokukabili?”

            Akasema; “ Baada ya kuokoka ilibidi niache njia fulani fulani ambazo zilikuwa zinanisaidia kupata fedha kwa kuwa zilikuwa ni kinyume cha maadili ya kikristo. Lakini sasa naona napata shida, sina fedha za chakula, wala sijui kodi ya nyumba mwezi huu nitapata wapi. Licha ya hayo, wale niliowakopa fedha kufanyia biashara hizo nilizoziacha wananidai fedha zao. Hata naogopa kukutana nao. Hebu nisaidie mawazo, najua nimeokoka kweli, lakini NITAISHIJE KATIKA HALI HII?”

            Unadhani swali lilikuwa jepesi kujibu? Si swala la kumwambia tuombe halafu umwache aende zake! Yeye anachotaka baada ya kuomba aone msaada unamjia. La sivyo maombi hayo yanakosa maana kwake.

            Swali hili “Nitaishije katika hali hii?” Linawasumbua walio wakristo wengi siku hizi. Na umefika wakati wa kulijibu.

            Ngoja nikuulize swali jingine. Unadhani mwanamke ambaye anafanya uasherati ili kupata fedha za kuwalishia watoto wake hajui kuwa uasherati ni dhambi? Nina uhakika anajua kwa kuwa kuna mwingine hata kama anafanya hayo hakosi kila jumapili kanisani, na wakati mwingine hutoa sadaka kwa fedha hiyo hiyo. Unadhani hajui kuwa uasherati ni dhambi? Unadhani hamwelewi mchungaji anaposema acheni dhambi? Unadhani haogopi magonjwa ya zinaa? Unadhani anapenda kufanya hivyo? Nina hakika walio wengi hawapendi kufanya hivyo. Lakini jambo linalomsumbua, akiacha uasherati atapata wapi fedha za kuwatunza watoto wake? Nina uhakika akijibiwa swali hili ni rahisi kuacha tabia hiyo chafu.

            Wasichana wengi mashuleni wamejikuta wamebeba mimba na kuharibu usichana wao kwa kudanganywa na fedha wanazozihitaji kwa ajili ya kununulia mafuta ya kupaka, nguo, na kutengeneza mitindo ya nywele.

            Vijana wengi wa kiume wamejikuta wamejiingiza katika biashara haramu kwa sababu ya kutaka utajiri wa haraka haraka.

            Kwa sababu ya kutokujua la kufanya wakristo wengi wamepoteza ushuhuda wao kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi.

            Wakristo wenzetu walifanyaje? Tusome kitabu cha Matendo ya Mitume 4:32,34,35.

            “Na jamii ya watu waliamini (Wakristo) walikuwa na MOYO MMOJA NA ROHO MOJA; wala hapana mmoja aliyesema ya kuwa kitu cho chote alicho nacho ni mali yake mwenyewe; bali walikuwa na VITU VYOTE SHIRIKA. WALA HAPAKUWA NA MTU MMOJA MIONGONI MWAO MWENYE MAHITAJI; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa; wakaiweka miguuni pa mitume, kila mtu akagawiwa KWA KADRI YA ALIVYOHITAJI”

            Utaona katika habari hii ya kuwa kwa sababu ya Ukarimu na kutokuwa na ubinafsi wakristo hao waliweza kupambana na tatizo la umaskini katikati yao. Ndiyo maana ikandikwa kuwa; “WALA HAPAKUWA NA MTU MMOJA MIONGONI MWAO MWENYE MAHITAJI”. Jina la Bwana libarikiwe!

            Matokeo ya usharika namna hii ni haya; “Na mitume wakatoa ushuhuda wa kufufuka kwake Yesu kwa nguvu nyingi, na neema nyingi ikawa juu yao wote” (Matendo ya Mitume 4:33)

            Je! Siku hizi hakuna wakristo wenye mahitaji kati yetu? Na tunafanya nini ili kuwasaidia? Je! Kuwaombea tu kunatosha? Je! Unashangaa kwa nini ushuhuda wa kufufuka kwake Yesu hautangazwi kwa nguvu na wakristo? Nadhani wakristo wengi wanatumia muda wao mwingi sana kujitafutia mahitaji yao kiasi ambacho muda unaobaki hautoshi kufanya kazi ya kushuhudia.

            Wenzetu walisaidiana, na sisi tusaidiane. Wazazi mara nyingi huwa wanawasaidia vijana wao waliowaoza kuanza maisha mapya. Na fahamu kuwa wokovu ni maisha mapya. Tunawajibika sana kuwasaidia wale wanaookoka kiroho na kimwili kuanza maisha mapya ndani ya Kristo. Kwa kukosa msaada wa kiuchumi, wengi wamepoa na kurudi nyuma.

            Niliwahi kushirikishwa ushuhuda mmoja ambao naamini utakusaidia kukuelewesha jambo hili ninalokuambia.

            Kuna mtu mmoja aliokoka baada ya muda mrefu kuwa mganga wa kienyeji na mchawi. Baada ya kuokoka ilibidi aache uchawi na uganga wa kienyeji, shughuli hizi ndizo zilizokuwa zinamsaidia kupata fedha ya matumizi.

            Baada ya kukaa miezi michache katika wokovu, bila ya kuwa na njia nyingine ya kupata fedha, ilibidi atumie akiba yote aliyokuwa nayo. Baada ya hiyo akiba kuisha akaanza kupata shida namna ya kuishi.

            Akiwa katika mahangaiko hayo, wakaja watu nyumbani kwake wakiomba msaada wa kutibiwa magonjwa yao. Hao watu walisikia kuwa yeye ni mganga wa kienyeji, wala hawakujua kuwa alikuwa ameokoka na kuacha uganga huo.

            Kwa sababu ya kukosa fedha, huyo mtu aliyeokoka akawaza moyoni mwake; “Hawa watu hawajui kuwa nimeokoka, kwa hiyo hakuna haja ya kuwaambia, kwani kuna ubaya gani nikienda kuwachimbia dawa ninazozifahamu halafu wanipe fedha inisaidie?”

            Kwa hiyo akaenda akawachimbia hizo dawa akawapa. Na hao watu wakaondoka baada ya kumlipa fedha. Lakini usiku, huyo aliyeokoka alipokuwa amelala aliona katika maono. Katika maono hayo akayaona majini mawili yaliyokuwa yanamsaidia katika uchawi zamani kabla ya hajaokoka. Hayo majini yakasema; “Tulikwaambia hutafanikiwa katika wokovu, sisi ndiyo tumekufilisi mali yako. Na pia sisi ndiyo tuliowatuma wale wagonjwa waje kwako. Ulipochima zile dawa ukatuita tulikokuwa. Sasa tumekuja, mwache Yesu njoo kwetu nasi tutakutajirisha”.

            Huyo mtu aliyeokoka aliposikia hayo, akatambua kosa lake, na mara hiyo akalikumbuka jina la Yesu Kristo. Kwa hiyo akayakemea yale majini nayo yakatoweka. Akamka akiwa anatetemeka.

            Kama asingelikumbuka uwezo wa jina la Yesu Kristo, angefanya nini? Naamini kama angepata msaada wa mahitaji yake toka kwa wakristo wenzake, asingebanwa na mtego huo. Wakristo naomba kuwakumbusha kusaidiana. Ni muhimu sana kwa maisha yetu ya kila siku.

            Ndiyo maana Mtume Paulo aliongozwa na Roho Mtakatifu kuandika hivi:

            “Kwa habari za kuwahudumia watakatifu (Wakristo) sina haja ya kuwaandikia. Maana najua utayari wenu, ninaojisifia kwa ajili yenu kwa Wamakedonia, kwamba Akaya ilikuwa tayari tangu mwaka mzima; na bidii yenu imewatia moyo wengi wao ……. Maana utumishi wa huduma hii hauwatimizii watakatifu (Wakristo) riziki walizopungukiwa tu, bali huzidi sana kuwa na faida kwa shukrani nyingi apewazo Mungu, kwa kuwa mkijaribiwa kwa utumishi huo, wanamtukuza Mungu kwa ajili ya utii wenu katika kuikiri Injili ya Kristo, na kwa ajili ya ukarimu wenu mliowashirikisha wao na watu wote” (2Wakorintho 9:1,2,12 – 15)

            Ndiyo maana pia katika makanisa kuna mgawanyiko wa huduma. Kuna wengine kazi yao ni kuhubiri na kuwaambia watu waache dhambi kama, uasherati na wizi. Ni wajibu wa wale wanaoshughulika na mambo ya miradi ya maendeleo katika kanisa ni kusaidiana na wahubiri hao kuwaongoza watu waishije baada ya kuacha uasherati na wizi.

            Napenda kukuhimiza hata wewe unayeyasoma haya kuwa, ukiona mwenzako ni mhitaji wa kitu fulani ambacho unacho, usisite kumsaidia. Kumbuka huduma hii ina thawabu yake kama Mtume Paulo anavyosema.

            Hebu jibu swali hili; “Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! Upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?" (1Yohana 3:17)

            Mzee Yohana anatushauri anasema, “Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli” (1Yohana 3:18).

            Ni kweli Bwana Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani alikuwa maskini, lakini baada ya kufufuka alirudishiwa utajiri wake. Ndiyo maana Mtume Paulo anazungumzia juu ya “……… utajiri wake Kristo usiopimika” (Waefeso 3:8). Na katika Wafilipi 4:19 tunasoma hivi; “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu”.

            Kumbuka ya kuwa; Yesu Kristo alichukua madhaifu yetu na magonjwa yetu yote, na kwa kupigwa kwake sisi tumepona (Isaya 53:5; Mathayo 8:16, 17; 1Petro 2:24). Na kwa kujua hili kanisa linajihusisha na kuombea wagonjwa na kutoa huduma za afya kwa wagonjwa.

            Kumbuka ya kuwa; Yesu Kristo alichukua dhambi zetu na akafanyika dhambi kwa ajili yetu, “Ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye” (2 Wakorintho 5:21). Na kwa kujua hili kanisa linahubiri habari za ondoleo la dhambi kwa ye yote atakayemwamini Kristo.

            Kumbuka ya kuwa; Yesu Kristo alikuwa maskini, ingawa alikuwa tajiri, ili kwa umaskini wake sisi tupate kuwa matajiri (2Wakorintho 5:21). Na kwa kujua hili kanisa linajihusisha na miradi mbalimbali ya kimaendeleo ili mtu aondokane na umaskini. Wakristo binafsi pia wanashauriwa kuwa na miradi isiyovunja maadili ya kikristo, ili waondokane na umaskini.

SADAKA NA WOKOVU

             “Palikuwa na mtu Kaisaria jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu SADAKA NYINGI, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na SADAKA ZAKO zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro. Yeye ni mgeni wa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi, ambaye nyumba yake iko pwani; ATAKUAMBIA YAKUPASAYO KUTENDA” (Matendo ya Mitume 10:1 – 6).

            Tabia hii ya Kornelio ya kuwa mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, na pia tabia ya utoaji wa sadaka na kumwomba Mungu daima, inaonyesha wazi kuwa Kornelio alimpenda Mungu sana na alikuwa anatafuta namna yakukubalika mbele zake na namna ya kumpendeza Yeye.

            Tungezungumza kwa lugha nyepesi zaidi, ni kwamba alitaka kwa MATENDO YAKE aende mbinguni na kuurithi Uzima wa Milele baada ya kufa kwake . Kwa kifupi alimtafuta Mungu kwa njia ya Matendo.

            Hii ina maana ya kuwa Kornelio alitaka kuvuna  baraka za Agano Jipya katika damu Yesu, wa kutumia njia za kupendeza Mungu zilizomo katika Agano la Kale.

            Tena ingawa yeye hakuwa Myahudi kwa kuzaliwa, alitaka sana kuvuna baraka ambazo Mungu aliahidi juu ya Wayahudi.

            Mpaka hivi leo kuna watu wengi wanataka kuvuna baraka toka kwa Mungu bila kutumia utaratibu aliouweka Mungu wa kuzipokea. Ni vigumu sana kupokea ahadi za Mungu nje ya mpango wake.

            Huwezi kupokea ahadi za agano la kale kwa kutumia mbini za agano la kale na huku sasa hivi tumo katika kipindi cha agano jipya.

            Baraka zote zilizomo katika agano la kale aliahidiwa Ibrahimu na uzao wake MILELE. Soma mwenyewe Mwanzo sura ya 17 na 22. Kwa hiyo ukitaka kupokea baraka za agano la kale lililofungwa kati ya Mungu na Ibrahimu, inabidi uwe mzao au mtoto wa Ibrahim. - Kornelio hakufahamu hili; hata leo hii wengi hawafahamu.

            Baraka zote zilizomo katika agano jipya zimeahidiwa wale walio ndani ya Kristo – waliotoa maisha yao kwa Yesu kama vile Yesu Kristo alivyotoa maisha yake kwa ajili yao.

            Ni vigumu kupokea baraka za ahadi za agano la kale na zile za agano jipya NJE YA YESU KRISTO. Imeandikwa hivi katika Wagalatia 3:13,14,29;

“Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, baraka ya Ibrahimu IWAFIKILIE MATAIFA KATIKA YESU KRISTO, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani…… Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi. "

  Ndiyo maana Mungu alimtuma Malaika wake ili amwambie Kornelio kuwa amwite Simon Petro ili awaeleze habari za Yesu Kristo – ili baraka ya Ibrahimu iwafikie na wapate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani –  SIYO KWA MATENDO PEKE YAKE.
            Jambo ambalo Mungu alitaka Kornelio ajue na sisi pia tujue ni kuwa matendo mema, maombi na SADAKA bila “kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani” yaani kuzaliwa mara ya pili kwa Roho au kuokoka – haitoshi  kumpendeza Mungu, wala kukubalika mbele zake au kuhesabiwa haki.

            Ndiyo maana Yesu Kristo alimwambia Nikodemo, yule Farisayo kuwa “Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu ….. Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, HAMNA BUDI kuzaliwa mara ya   pili”(Yohana 3:3,7).

            Haya maneno “Hamna Budi” maana yake ni “lazima” kwa hiyo Yesu Kristo alikuwa anasema “…… LAZIMA kuzaliwa mara ya pili”.

            Yesu Kristo alikuwa anasisitiza kwa Nikodemo, na hata kwetu sote tunaotaka kuurithi ufalme wa Mungu, kuwa hakuna njia nyingine isipokuwa LAZIMA kuzaliwa mara ya pili kwa Roho (au kwa maneno mengine) LAZIMA Kuokoka!

IMANI NA MATENDO

                  Matendo peke yake hayatoshi kukupa ufalme wa Mungu. Kuna watu wengi sana ambao ni waaminifu sana katika kusali na kumtolea Mungu sadaka, lakini hawakubaliani na jambo kuokoka. Wanaona kuwa wao tayari wameokoka kwa sababu tu wanasali, wanatoa sadaka na kujitahidi kuishi katika matendo mema. Hebu soma   maneno ya mistari hii uone yanavyopingana na msimamo huu;

“Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; WALA SI KWA MATENDO, mtu awaye yote asije akajisifu” (Waefeso 2:8,9)

          Tunaokoka kwa njia ya imani itendayo kazi katika Yesu Kristo, “Wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu”. Matendo yana faida zaidi kwa mtu baada ya kuokoka. Na pia imani bila matendo, imani hiyo imekufa nafsini mwake. Biblia inasema hivi:

           “Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo? Je! ile imani yaweza kumwokoa?…. Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake. Lakini mtu atasema, wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha IMANI YANGU KWA NJIA YA MATENDO YANGU …….. Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa” (Yakobo 2:14,17,18,26).

                  Jambo ambalo Yakobo alikuwa anasisitiza hapa ni kutaka kuwaonya watu kuwa kusema wewe ni mkristo na huku matendo yako hayalingani na ushuhuda wa mdomo wako ni bure. Wokovu uonekane katika maisha yetu kila siku – la sivyo imani tuliyo nayo inakosa kuzaa matunda ya uzima wa milele. Ndiyo maana Yesu Kristo aliwahi kuzungumza juu ya kukatwa kwa tawi (Mkristo) lisilo zaa, soma Yohana 15:1-8 ili upate picha zaidi juu ya jambo hili.

CHUKUA HATUA LEO

          Malaika alimwambia Kornelio atume watu wakamwite Simoni aitwaye Petro ili AMWAMBIE YAMPASAYO KUTENDA. Mungu kwa uweza wa Roho wake Mtakatifu amekuletea maneno haya mkononi mwako ili UFAHAMU YAKUPASAYO KUTENDA.

          Kama hujaokoka na unadhani unaweza kuokoka kwa kutoa sadaka nyingi NAKUSHAURI KWA JINA LA YESU KRISTO WA NAZARETI uombe sala hii kwa sauti, ili utubu na kumpa Yesu Kristo maisha yako leo. HALAFU endelea kutoa sadaka nyingi ukiwa ndani ya Yesu Kristo.

          Omba sala hii kwa sauti; “Mungu Baba, unisamehe dhambi zangu zote nilizokukosea katika maisha yangu. Ninatubu kwako. Nitakase kwa damu ya Yesu Kristo. Bwana Yesu Kristo nimefungua moyo wangu nakukaribisha uingie ndani yangu, kwa uwezo wa Roho wako. Uwe Bwana na Mwokozi wa maisha yangu – sasa na hata milele. Asante kwa kunisamehe dhambi na kuniokoa. Amina”.

          Ikiwa umeisema sala hii kwa uaminifu, basi umefanyika kiumbe kipya – umezaliwa mara ya pili na Mungu hakumbuki dhambi zako tena. Soma 2Wakorintho 5:17, Waebrania 8:12. Karibu sana katika ufalme wa Mungu kwa jina la Yesu Kristo!

          Hili ndilo lililotokea kwa Kornelio na jamaa yake, Simoni Petro alipofika kwao aliwaambia habari za Yesu Kristo – walisikia maneno hayo wakamwamini Yesu na kujazwa na nguvu za Roho Mtakatifu wakati huo huo.

UCHUMI WA UFALME WA MBINGUNI

Mama mmoja aliyekuwa na watoto sita (lakini alikuwa hajaolewa), alipelekwa na mwenzake kwa Askofu wa dhehebu lao ili wapate msaada kwa kuwa walikuwa na maisha ya shida sana. Yule mama pamoja na watoto wake sita walikuwa wanakaa katika nyumba ya makaratasi, na hawakuwa na chakula cha kutosha.

Askofu alimuuliza yule mama amewapateje wale watoto wote sita na huku alikuwa hajaolewa.

Yule mama akajibu akasema; "Mtoto wa kwanza nilimpata kwa kuwa nilikuwa nataka mtoto, niliona nazeeka bila ya kuolewa nikaona nizae mtoto, Lakini mtoto wa pili nilimpata wakati nilipokuwa natafuta chakula cha mtoto wa kwanza. Mtoto wa tatu nilimpata nilipokuwa natafuta chakula cha watoto wawili niliokuwa nao. Na hali hii imeendelea mpaka sasa nina watoto sita – na sijui nitaendelea na hali hii mpaka lini".

Ni wazi kabisa si mapenzi ya Mungu huyu mama aishi maisha ya namna hiyo. Vikwazo vya uchumi ambavyo vilimzunguka yule mama na watoto wake vilitoka kwa ibilisi.

"Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa ……." (Hosea 4:6). Maneno haya yaliyosemwa na Mungu kwa kinywa cha Nabii Hosea yana ukweli ndani yake hata hivi leo. Watu wengi sana siku hizi wanaangamizwa, wanadhulumiwa, wanahuzunishwa na maisha kwa sababu tu wamekosa kuyajua maarifa ya Mungu yaliyomo katika Neno lake.

Wakati fulani nilikuwa nafundisha katika semina moja juu ya uhusiano wa maendeleo ya mtu na Wokovu, na wakati wa kipindi cha majadiliano Mchungaji mmoja akatueleza habari iliyotufikirisha sana.

Akasema ya kuwa katika kanisa alilokuwa analihudumia miaka ya nyuma aliwahi kufuatwa na mama mmoja wa usharika huo ambaye alikisema ya kuwa yeye alikuwa mmoja wa wakina mama thelathini ambao hawashiriki chakula cha Bwana kwa kuwa walikuwa wanaishi hapo mjini kwa njia za umalaya. Ombi lao kwa mchungaji wao lilikuwa ni kwamba akiweza kuwasaidia kupata kazi za halali waache umalaya. Wao wametafuta kazi bila ya mafanikio, na wanafanya umalaya si kwa sababu wanapenda, bali kwa kuwa hawakuwa na njia nyingine ya kupatia fedha.

Ni jambo la kumshukuru Mungu, ya kuwa mchungaji yule aliweza kuwatafutia kazi wale wakina mama wote katika kiwanda kimoja, na maisha yao yakabadilika wakaacha umalaya, na kuishi maisha ya kikristo yenye ushuhuda.

Ni watu wangapi ambo wanaishi maisha yao kinyume na maadili ya kikristo ili kupata fedha za kuwasaidia kila siku? – Ni wazi kuwa ni wengi. Je! hawawezi wakapata riziki yao bila kudhulumu au kuiba au kudanganya au kuzini? – Ni wazi kuwa wanaweza. Sasa, ni kwa nini wanaishi kwa jinsi hiyo?

Jambo ambalo watu wanahitaji kujua ni kuwa baba wa uongo yaani shetani amewadanganya kwenye mawazo ya kuwa hakuna njia nyingine ya halali ya kupatia fedha isipokuwa hizo. Na shetani anausimamia uongo huo ili uonekane kuwa ni kweli kwa kuwawekea watu hasa wakristo vikwazo vigumu vya kiuchumi.

Unaweza ukawa unajiuliza vikwazo hivyo ni vipi? Vikwazo hivi vinatofautiana katika watu mbalimbali na mahali mbalimbali. Kuna watu wengine wataona hakuna mradi wa halali wanaoufanya unaofanikiwa. Mwingine miradi yake inafanikiwa, lakini fedha yote inaishia kutafutia matibabu ya magonjwa yaliyomo ndani ya nyumba yake ambayo hayaishi.

Mwingine anapata magari mengi, lakini hayaishi kupata pancha na kuharibika au kuanguka. Mara nyingi utawasikia watu wa jinsi hii wanasema wana mkosi. Kwa kweli si mkosi bali vikwazo vya kiuchumi toka kwa shetani ili ushindwe maisha na UANZE KUTAFUTA MAISHA MAZURI KWA NJIA ZILIZO KINYUME NA MAADILI YA KIKRISTO YALIYO MATAKATIFU.

Jambo ambalo wakristo wengi hawalifahamu

Mimi na mke wangu miaka ya mwanzo tulipookoka hasa mwaka 1984 na 1985 tulikumbana na vikwazo vigumu sana vya kiuchumi. Tuliona jinsi maisha yalivyokuwa yanarudi nyuma – fedha tuliishiwa, chakula tuliishiwa, nguo tuliishiwa, vitu ndani vilianza kuharibika na hatukuwa na fedha za kuvitengenezea. Tulijaribu kulima bustani za mboga, hazikufanikiwa. Tulijaribu kupika chapati za kuuza, hazikununuliwa zikaharibika tukazitupa.

Kwa kifupi tuliona maisha ya wokovu kuwa ni magumu, ya shida na ya kimaskini sana. Tulishindwa hata namna ya kuwasaidia ndugu zetu vizuri. Hali hii ilitutia uchungu sana. Watu hawakufahamu ya kuwa hali hii ilikuwa inatunyima amani ya kweli ya wokovu – kwa kuwa tulijitahidi kuwachangamkia wote ili kuficha mapambano tuliyokuwa nayo kimaisha.

Ilikuwa ni vigumu sana kuishi maisha ya ushuhuda mzuri wa kikristo katikati ya mahitaji makubwa kama hayo tuliyokuwa nayo.

Tulijua kuwa Zaburi 23:1 inasema, "Bwana ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu". Lakini tulikuwa tumepungukiwa na vitu vingi vya lazima katika maisha. Hatukufahamu kwa nini sisi kama kondoo wa Kristo tulikuwa tumepungukiwa namna hiyo!

Tulikuwa tunasoma lakini tunashindwa kumwelewa Mtume Paulo alipokuwa anasema katika Wafilipi 4:12 kuwa; "najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa".

Tuliona ya kuwa Mtume Paulo aliweza kuwa na amani na ushindi katika hali yo yote aliyokuwa nayo – hata katika upungufu. Sisi tulikosa amani tulipokuwa tumepungukiwa! Na hili jambo lilitusumbua sana.

Tulikuwa tunafurahi tunaposoma mstari kama ufuatao; " …..vyote ni vyenu …. Vile vilivyopo sasa, au vile vitakavyokuwapo; vyote ni vyenu, nanyi ni wa Kristo, na Kristo ni wa Mungu" (Wakorintho 3:21,22). Tulikuwa tunafurahi kwa kuwa maneno haya yanatupa uhalali wa kumiliki vitu vilivyo vya Mungu. Kwa mfano Hagai 2:8 inasema "Fedha ni mali yangu, na dhahabu ni mali yangu, asema Bwana wa Majeshi." Pia, Zaburi 24:1 inasema "Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana …" Lakini jambo lililotusumbua ni kwamba ingawa mistari hiyo ilitupa umilikaji juu ya fedha, dhahabu na vyote viijazavyo nchi ili tuvitumie – SISI HATUKUWA NAVYO WALA HATUKUJUA TUTAVIPATAJE!

Tulifahamu ya kuwa ni mapenzi ya Mungu tufanikiwe katika mahitaji ya kiroho na mahitaji ya mavazi, chakula, na malazi; soma kitabu cha 3 Yohana 1:2. Kwa hiyo tulikuwa na hamu kubwa ya kufanikiwa.

Tulitamani sana kuona maneno ya Wafilipi 4:19 yanatimia kwetu – nayo yanasema hivi;

"Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu".

Hali hii ilitufanya tuingie katika maombi mazito, ili kumuuliza Mungu njia na namna ya kuondokana na hali tuliyokuwa nayo.

Mambo makubwa matatu yafuatayo, Roho wa Mungu alituambia kuwa ni chanzo cha matatizo yaliyokuwa yanatukabili: Alituambia yafuatayo:

Kuwa, ingawa tumezaliwa mara ya pili na kuingizwa katika ufalme wa Mungu – tulikuwa bado tunategemea utaratibu wa uchumi wa duniani badala ya kutumia na kutegemea utaratibu wa uchumi wa mbinguni;

Kuwa, tulikuwa tunapenda kupokea bila ya kuwa watoaji, na pia tulitaka kuvuna tusichokipanda. Roho Mtakatifu aliuliza swali, Je! unaweza kwenda kwenye bustani yako kuchuma nyanya huku ukijua kuwa hujawahi kupanda nyanya? Ni wazi kuwa jibu lilikuwa ni hapana.

Kuwa, hatujafahamu ya kuwa adui yetu ibilisi ndiye chanzo cha mahangaiko na mafadhaiko yaliyoambatana na kupungukiwa mahitaji katika maisha. Na pia tulikuwa hatutumii silaha tulizopewa ili kuzivunja kazi za ibilisi katika maisha yetu.

Baada ya kupokea majibu hayo kutoka kwa Mungu, tulitubu na kuomba msamaha. Tuliendelea kumwomba Mungu atufundishe na atuongoze katika kuishi maisha ya kutumia na kutegemea utaratibu wa uchumi wa ufalme wa mbinguni.

Mafundisho tuliyoyapata yalituondoa katika mahangaiko ya kupungukiwa na kutuingiza katika furaha na amani ya mafanikio NDANI YA KRISTO.

Ndiyo maana tumechukua hatua hii chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu kukushirikisha baadhi ya mafundisho hayo ili ikiwa umo katika hali ya mahangaiko ya kupungukiwa na mahitaji muhimu ya maisha upate msaada wa kuondokana nayo.

Kumbuka ni mapenzi ya Mungu ndani ya Kristo kuwa ufanikiwe na uishi maisha ya ushindi katika maeneo yote ya maisha yako na katika siku zote utakazoishi juu ya nchi.

Mwenye haki ataishi kwa imani

Nabii Habakuki aliishi katika kipindi kilichokuwa kigumu sana kiuchumi. Hali hii iliwafanya watu wengi kuingia katika dhuluma, udanganyifu na mambo mengine maovu ili tu waweze kuishi.

Lakini kilichoumiza moyo wa Nabii Habakuki ni kuona kuwa kulikuwa na watu wachache ambao hawakufuata mambo maovu – lakini waliishi maisha magumu na kuonewa na matajiri wa wakati huo. Hali hii ilimfanya Nabii Habakuki aingie katika maombi ya kumlalamikia Mungu, huku akihitaji kujua mpango wa Mungu juu ya watu waliosimama upande wake. Soma kitabu cha Habakuki sura ya 1 na 2.

Kati ya jibu ambalo Mungu alimpa Nabii Habakuki juu ya maisha ya watu wake katikati ya hali ngumu ya uchumi ni maneno haya;

"….mwenye haki ataishi kwa imani yake" (Habakuki 2:4)

Huu ndio uliokuwa mpango wake kwa watu wake wakati ule ili uwasaidie kuishi katikati ya dhuluma na maovu yanayotokana na hali ngumu ya uchumi.

Katika siku hizi za mwisho, kumetabiriwa kutokea tena hali ngumu ya uchumi inayoambatana na dhuluma pamoja na maovu mbalimbali. Mungu amekwisha andaa mpango mzuri kwa ajili ya wote watakaoipokea na kuikiri injili ya Kristo inayookoa. Na mpango huu ni sawa na ule aliopewa Nabii Habakuki.

Kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, Mtume Paulo alisema maneno muhimu yafuatayo:

" Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia. Kwa maana haki ya Mungu inadhihirishwa ndani yake, toka imani hata imani; kama ilivyoandikwa , MWENYE HAKI ATAISHI KWA IMANI" (Warumi 1:16-17).

Huu ndio mpango wa Mungu kwa watu wote wanoipokea Injili ya Kristo na kuokolewa. Katikati ya dhuluma,wizi, uasherati na maovu mbalimbali yanayoambatana na hali ngumu ya uchumi iliyopo sasa na ile itakayotokea miaka si mingi iliyo mbele yetu kuanzia sasa – Mungu anawataka watu waishi kwa kufuata mpango wake – WAISHI KWA IMANI.

Kuishi kwa Imani ndiyo utaratibu wa uchumi wa mbinguni ambao kila mkristo anatakiwa kuufuata akitaka kuishi maisha ya mafanikio na matakatifu katikati ya hali ngumu ya uchumi – badala ya kujikuta amewezwa na masumbufu ya maisha haya.

Inasikitisha kuona kuwa wakristo wengi wameyatafsiri na kuyatumia vibaya maneno haya "kuishi kwa Imani". Na kwa ajili hiyo mpango wa Mungu uliomo ndani ya maneno haya haujaeleweka na wengi.

Wakristo wengine wanafikiri kuishi kwa imani ni kuacha kazi wanazozifanya na kuanza kuishi maisha ya omba omba na ya kubahatisha. Wamesahau kuwa biblia inasema mtu asipofanya kazi asile – soma 2Wathesalonike 3:6 – 12.

Ingawa kuna wakristo ambao wamelifanya neno hili "kuishi kwa Imani" lisieleweke vizuri; hali hii haiwezi wala haitaweza kubadilisha mpango wa Mungu uliomo ndani yake.

Mawazo yetu siyo mawazo ya Mungu; njia zetu si njia za Mungu; na mipango yetu si mipango ya Mungu. Hakuna njia ya mkato kwa mkristo safi ya kufanikiwa katika maisha, isipokuwa ni kwa kuishi ndani ya mpango wa Mungu uliofunuliwa katika Kristo Yesu.

"Mwenye haki ataishi kwa imani" maana yake nini? "Mwenye haki" maana yake Mkristo, au Mtakatifu, au Mwongofu, au Mteule, au Aliyeokoka. Kwa hiyo tunaweza kusema Mkristo ataishi kwa imani.

Pia tunasoma katika Waebrania 11:1 ya kuwa:"Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana"

Tena imeandikwa katika Warumi 10:17 ya kuwa;"Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo".

Tena imeandikwa katika Yakobo 2:26 ya kuwa;"Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa".

Kwa mistari hiyo michache na mingine mingi iliyomo katika Biblia inatusaidia kujua ya kuwa "Mwenye haki ataishi kwa imani" maana yake kila mkristo anatakiwa kuishi kwa kuwa mtendaji wa Neno la Kristo na siyo msikiaji tu – kila wakati na katika kila eneo la maisha yake.

Roho Mtakatifu alipokuwa anatufundisha haya mimi na mke wangu, tulijua hakika ya kuwa tunatakiwa kutumia muda mwingi kulisoma na kulitafakari Neno la Kristo, ili tuweze kulitenda Neno hilo katika maisha haya. Tulianza kusoma Neno la Mungu na vitabu mbalimbali vilivyoandikwa na watumishi wa Mungu na bado tunaendelea kufanya hivi hata leo, na tumeona mabadiliko makubwa katika maisha yetu – maana mahangaiko tuliyokuwa nayo yametoweka kwa jina la Yesu Kristo! Sasa tunaishi katika maisha ya ushindi na amani ndani yake Kristo.

Tatizo ambalo mtu analipata anapookoka, ni namna ya kuishi katika maisha mapya ya wokovu (2Wakorintho 5:17)

Biblia inatuambia ya kuwa sisi ni raia wa nyumbani mwake Mungu (Waefeso 2:19). Pia inatuambia kuwa sisi si wa ulimwengu huu (Yohana 17:14). Kwa hiyo maisha yetu hayatakiwi kuongozwa na utaratibu wa hapa duniani.

Kuna tofauti kati ya utaratibu wa uchumi wa duniani na utaratibu wa uchumi wa ufalme wa mbinguni. Ingawa sisi tulio wake Kristo tumo humu ulimwenguni hatutakiwi kuishi kwa kutegemea utaratibu wa uchumi wa dunia hii unaoyumba, bali tutegemee utaratibu wa uchumi wa ufalme wa mbinguni – usioyumba wala kubadilikabadilika kwa kuwa umejengwa juu ya mwamba imara – Neno la Kristo.

Wakristo wengi kwa kutokujua hili wamejikuta wakipata shida ya kutaka kuwatumikia mabwana wawili – yaani Mungu na Mali ambapo Yesu Kristo alikwishasema haiwezekani. Matokeo yake ni kupoteza ushuhuda wa kikristo na kuishi maisha ya mahangaiko.

Kutegemea utaratibu wa uchumi wa dunia hii kuna shida sana kwa kuwa uchumi huo ukiyumba kidogo, na wewe unayumba kimaisha. Lakini ukiutegemea utaratibu wa uchumi wa ufalme wa mbinguni huwezi kuyumba wakati uchumi wa dunia ukiyumba – kwa kuwa tumaini lako halimo mikononi mwa dunia na wanadamu – bali ndani ya Kristo Yesu ambaye ni mwamba imara usiotikisika.

Katika sura zifuatazo nitaelezea mambo mbali mbali muhimu yaliyomo katika utaratibu au mfumo wa uchumi wa ufalme wa mbinguni. Kwa hiyo usiache kusoma mfululizo wa somo hili katika sura zinazofuata baada ya kila wiki.

TOFAUTI YA ZAKA NA DHABIHU

                  Kutokutoa zaka na dhabihu ni kumwibia Mungu. Mtu aliye mkristo asipotoa zaka na dhabihu anaitwa mwizi. Kuna wakristo ambao ni wezi lakini wao hawajui yakuwa ni wezi. Wamemwibia Mungu zaka na dhabihu. Mungu anasema hivi:

             “Je! mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi. Lakini ninyi mwasema, tumekuibia kwa namna gani? Mmeniibia ZAKA na DHABIHU” (Malaki 3:8)

          Kati ya amri tulizopewa na Mungu ni kwamba tusiibe. Kuiba ni dhambi. Na dhambi ina adhabu yake. Popote palipo na dhambi, laana hutokeza. Kwa wale wanaomwibia Mungu kwa kutokutoa zaka na dhabihu, wamefunikwa na laana. Ndiyo maana Mungu alisema hivi:

                “….. Mmeniibia Zaka na Dhabihu. Ninyi mmelaaniwa kwa laana;   maana mnaniibia mimi, naam, taifa hili lote  (Malaki 3:8b, 9).

          Laana maana yake ni kutokufanikiwa, kutofaulu, kutokustawi, kukosa furaha, kukosa amani, na kukosa mwelekeo sahihi. Ni wazi kuwa wakristo wengi hawana furaha, hawana amani na hawafanikiwi katika maisha yao ya kila siku, kwa sababu hawamtolei Mungu zaka na dhabihu.

            Unapokosa kumtolea Mungu ili ujenzi wa nyumba yake – kanisa uendelee, Hagai 1:6 anatuambia Mungu anasema hivi;

            “Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo lakini hapana aonaye moto; na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka”.

Zaka ni kitu gani?

            Zaka ni fungu la kumi la pato lako. Hebu isome na kuitafakari mistari ifuatayo;

           “Tena zaka yote ya nchi, kama ni mbegu ya nchi, au kama ni matunda ya nchi, ni ya Bwana, ni takatifu kwa Bwana ….Tena zaka yote ya ng’ombe, au ya kondoo, kila apitaye chini ya fimbo; SEHEMU YA KUMI watakuwa ni watakatifu kwa Bwana” (Mambo ya Walawi 27:30 –32).

            “…Toa fungu la kumi lote la maongeo yako ya mwaka huo, uliweke ndani ya malango yako; na Mlawi kwa kuwa hana fungu wala urithi pamoja nawe, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe, walio ndani ya malango yako, na waje wale na kushiba; ili kwamba Bwana, Mungu wako,  akubarikie katika kazi yote ya mkono wako uifanyayo”(Kumbukumbu la Torati 14:28-29).

          Zaka ni fungu la kumi la pato toka mshahara wako ofisini, shambani au kwenye mifugo. Tena zaka hii ni ya Bwana na ni Takatifu.

                  Mtu asipoitoa zaka hii anamwibia Mungu. Zaka si yako hustahili kukaa nayo wala kuitumia nje ya utaratibu wa Mungu.

                  Lakini Malaki 3:10a anasema; “Leteni zaka KAMILI ….” Maana yake nini maneno haya? Maana yake ni hii; ikiwa kwa mfano mshahara wako kwa mwezi ni shilingi 2,000/= ( kabla ya makato) – fungu la kumi au zaka unayotakiwa kutoa ni shilingi 200/= ambayo ndiyo zaka kamili ya mshahara wako. Ukileta pungufu yake hiyo si zaka kamili.

                       Tena kwa mfano umevuna magunia 10 ya mahindi toka shambani mwako – zaka kamili unayotakiwa kutoa ni gunia moja bila kupungua. Kumbuka mzaliwa wa kwanza wa mifugo yako ni wa Bwana.

                      Unaweza ukasema habari za kutoa zaka ni za agano la kale na siyo za agano jipya.

          Waebrania 7:5-10 inatuambia wazi ya kuwa Ibrahimu alitoa fungu la kumi. Kama Ibrahimu alitoa sehemu ya kumi, Je! si zaidi sana kwetu sisi tulio uzao wake kwa imani ndani yake Kristo? Maana imeandikwa hivi;

            “Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu na warithi sawasawa na ahadi” (Wagalitia 3:29). Soma pia Wagalitia 3:13,14).

Dhabihu ni kitu gani?

          Dhabihu ni matoleo yanayotolewa baada ya kutoa sehemu ya kumi ya pato lako. Kwa mfano, kama mshahara wako kwa mwezi ni shilingi 2,000/=, basi sehemu ya kumi (zaka) ni shilingi 200/=. Kiasi cho chote utakachotoa ju ya shilingi 200/= ndiyo matoleo yako. Kwa mfano ukitoa shilingi 210/= toka kwenye mshahara wako wa shilingi 2000/=, Basi, shilingi 200/= ni zaka; na shilingi 10/= ni dhabihu au matoleo au sadaka ya kawaida.

          Kiasi utakachotoa katika dhabihu/matoleo, ndicho kitakachokuwa kipimo kitakachoweka kiwango chako cha kupokea. Imeandikwa hivi:

            “Lakini nasema neno hili, APANDAYE HABA ATAVUNA HABA; APANDAYE KWA UKARIMU ATAVUNA KWA UKARIMU. Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, MKIWA NA RIZIKI ZA  KILA NAMNASIKUZOTE,mpatekuzidisanakatikakilatendojema;kamailivyoandikwa, Ametapanya, amewapa maskini, haki yake yakaa milele. Na yeye ampaye mbegu mwenye kupanda, na mkate uwe chakula, atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye ATAYAONGEZA MAZAO YA HAKI YENU, MKITAJIRISHWA KATIKA VITU VYOTE MPATE KUWA NA UKARIMU WOTE; umpatiao Mungu shukrani kwa kazi yetu. Maana utumishi wa huduma hii HAUWATIMIZII WATAKATIFU RIZIKI WALIZOPUNGUKIWA TU, Bali huzidi sana kuwa na faida kwa shukrani nyingi apewazo Mungu; kwa kuwa mkijaribiwa kwa utumishi huo, WANAMTUKUZA MUNGU kwa ajili ya utii wenu katika kuikiri Injili ya Kristo, na kwa ajili ya ukarimu wenu mliowashirikisha wao na watu wote” (2Wakorintho 9:6-13)

          Soma tena mistari hiyo hapo juu, lakini sasa tafakari zaidi maneno niliyoyaandika kwa herufi kubwa. Utaona kuwa usipokuwa mwaminifu katika utoaji, wewe mwenyewe unakosa kufanikiwa, na pia unamkosesha Mungu shukrani na utukufu ambao angepata kwa utoaji wako.

Zaka na dhabihu zitolewe wapi?

          Hili jambo linahitaji uongozi wa Roho Mtakatifu, ili upate ufahamu Mungu anataka upeleke wapi zaka na matoleo uliyo nayo.
          Hili ni muhimu kwa kuwa Biblia inazungumza juu ya kupeleka kanisani (Malaki 3:10-11), kwa watakatifu (2Wakorintho 9:12), kwa maskini (2Wakorintho 9:8-9), kwa watumishi wa Mungu (1Wafalme 17:10-24; 1Wakorintho 9:7-14); kwa wajane, - na kadhalika.

              Muombe Mungu akuongoze mahali pa kupeleka. Amani ya Kristo na iamue moyoni mwako.

Baraka Tele!

          Kuna baraka tele za mafanikio kwa mkristo aliye mwaminifu katika kumtolea Mungu zaka na matoleo.

          Katika Malaki 3:10 imeandikwa hivi; “Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo (YA UTOAJI) asema Bwana wa Majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na KUWAMWAGIENI BARAKA, HATA ISIWEPO NAFASI YA KUTOSHA AU LA”.

           Je! umewahi kukutana na mkristo ambaye anashuhudia kuwa Mungu amempa baraka nyingi hata HANA MAHALI PA KUZIWEKA? Ni wazi kuwa ahadi hii haijatimia kwa kuwa hatujawa watendaji na Neno kikamilifu katika utoaji.

              Soma mistari hii hapa chini uone baraka zingine zinazotokana na utoaji; “Azaria Kuhani Mkuu, wa nyumba ya Sadoki, akamjibu, akasema, Tangu watu walipoanza kuleta matoleo nyumbani kwa Bwana, tumekula na KUSHIBA NA KUSAZA TELE; kwa kuwa Bwana amewabariki watu wake; na kilichosalia ndiyo akiba hii kubwa. Ndiko Hezekia akaamuru kutengeneza vyumba nyumbani mwa Bwana; wakavitengeneza. Wakayaingiza MATOLEO na ZAKA na vitu vilivyowekwa wakfu, kwa uaminifu ….” (2Mambo ya Nyakati 31:10-12).

          Kwa nini wakristo wengine wanapungukiwa vyakula, wakati tuna nafasi ya kumruhusu Mungu kutubariki kwa vyakula tele? Mpe Mungu nafasi ya kukubariki kwa kumtolea zaka na matoleo!

Anza Sasa!

             Nakushauri ya kuwa kama ulikuwa hutoi sehemu ya kumi au zaka pamoja na  matoleo ya kutosha – anza sasa.

             Jambo la kwanza, kumbuka kutubu kwa Mungu katika Jina la Yesu Kristo kwa kuwa ulimwibia zaka na dhabihu kwa kutokumtolea.

          Halafu mwombe Mungu akuwezeshe kusimama katika uaminifu wa kumtolea zaka na dhabihu ili apate nafasi ya kukubariki zaidi kama tulivyoona, na kama alivyoahidi.

 

 

UKITOA TEGEMEA KUPOKEA

            Sehemu nyingi nilizotembelea nimeona na kufahamu ya kuwa watu wengi wanatoa sadaka – fedha taslimu au vitu au wanyama kwa Mungu BILA KUTEGEMEA KUPOKEA KUTOKA KWA MUNGU.

          Furaha ya utoaji inatokana na kufahamu matokeo ya utoaji huu. Ndiyo maana mkristo yuko tayari kuweka shilingi 10,000/= katika mradi utakaompa faida kuliko kutoa kanisani ambako anafikiri sadaka hiyo haina faida kwake binafsi. Kwa hiyo siku zote atatoa sadaka kidogo kanisani au kwenye kazi ya Mungu.

            Bila ya mkristo kujua kwamba anajua na kuwa na uhakika moyoni mwake kuwa akitoa sadaka anastahili kupokea ZAIDI YA KIWANGO ALICHOTOA KUTOKA KWA  MUNGU – utoaji wake utakuwa chini siku zote.

            Wakristo wengi wanafikiri wakimtolea Mungu kitu, watazidi kupungukiwa na kufilisikia. Lakini ukweli wa mambo ni kwamba ukimtolea Mungu ulicho nacho UNAFUNGUA MLANGO WA KUFANIKIWA kwa ulivyo navyo. Unapomtolea Mungu hufilisiki bali unatajirika!

             Tunapokuwa ndani ya Kristo, tunachukua na kubeba tabia ya Mungu ndani yetu. Imeandikwa hivi:

“ Bali wote waliompokea(Kristo) aliwapa UWEZO wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake” (Yohana 1:12) “ Kwa kuwa UWEZA wake wa UUNGU umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe” (1Petro 1:13)

        Ni vizuri ufahamu ya kuwa mojawapo ya tabia ya Uungu tuliyo nayo ndani yetu katika Kristo ni tabia ya kutoa HUKU UKITEGEMEA KUPOKEA. Mungu akitoa kitu anategemea kupokea.

Tabia ya Mungu ya Utoaji

            Mungu alipokuwa anamtoa mwana wake wa pekee, alimtoa huku akitegemea kupata watoto wengi wa kiroho. “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanae pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele” (Yohana 3:16)
            Mungu alipokuwa anamtuma Roho Mtakatifu juu ya wanafunzi wake, alimtoa huku akitegemea kupata mashahidi wengi watakaosimama upande wake na kulitetea jina lake hapa duniani. “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalem, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi” (Matendo ya Mtume 1:8)
            Mungu anapotoa utajiri kwa watu wake, anautoa huku akitegemea kupata agano lililo imara kati yake na wanadamu. “ Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako,kama hivi leo” (Kumbukumbu la Torati 8:18).
            Hii ndiyo tabia tuliyo nayo ndani ya Kristo, kutoa huku tukitegemea kupokea. Hili jambo la kutoa na kupokea wakati mwingine linajulikana kama KUPANDA na KUVUNA.
            Hakuna mkulima anayepanda mbegu shambani bila kutegemea kuvuna. Kama hana tegemeo la kuvuna, basi hata haja na hamu ya kupanda inapotea – inakuwa haina maana kupanda maana hatapata kitu.
            Katika mambo ya kiroho ni vivyo hivyo. Utakachotoa ndicho utakachopata. Utakachopanda ndicho utakachovuna. Ukipanda fedha utavuna fedha. Ukipanda upendo utavuna upendo. Ukipanda ng’ombe utavuna ng’ombe. Ukitoa vitabu utapokea vitabu. Imeandikwa hivi; “ Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna” (Wagalatia 6:7).
            Hivi ndivyo ilivyo, utakachopanda ndicho utakachovuna. Kwa maneno mengine, ni kwamba ukipanda tegemea kuvuna.

Tumia tabia ya Mungu iliyo ndani yako

            Ikiwa wewe unakaa ndani ya Kristo na Kristo anakaa ndani yako, basi uwe na uhakika ya kuwa tabia ya Uungu ya kutoa na kupokea, kupanda na kuvuna imo ndani yako.
            Inaonekana wazi ya kuwa wakristo wa kanisa la Korintho na Filipi katika nyakati za huduma ya Mtume Paulo – walishiriki sana katika habari hii ya kutoa na kupokea. Siyo kutoa bila kupokea bali kutoa na kupokea. Hii ni tabia iliyoonekana wazi katika ukristo wao. Hebu soma maneno yafuatayo juu ya habari hii katika kitabu cha Wafilipi katika nyakati za huduma ya Mtume Paulo – walishiriki sana katika habari hii ya kutoa na kupokea. Siyo kutoa bila kupokea bali kutoa na kupokea. Hii ni tabia iliyoonekana wazi katika ukristo wao. Hebu soma maneno yafuatayo juu ya habari hii katika kitabu cha Wafilipi 4:10-14;

            “ Nalifurahi sana katika Bwana, kwa kuwa sasa  mwisho mmehuisha tena fikra zenu kwa ajili yangu,    kama vile mlivyokuwa mkinifikiri hali yangu; lakini mkupata nafasi. Si kwamba nasema haya kwa kuwa  nina mahitaji; maana nimejifunza kuwa radhi na hali  yo yote niliyo nayo. Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefudishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu. LAKINI MLIFANYA VEMA, mliposhiriki nami katika dhiki yangu”.

            Mtume Paulo hapa anawaambia Wafilipi wazi kuwa maisha yake yote na katika mambo yote na katika hali yo yote tumaini lake na ushindi wake ni katika UWEZA WA KRISTO amtiaye nguvu – na wala si katika uweza wake Paulo au huruma za wanadamu. Hata hivyo aliwaambia “MLIFANYA VEMA MLIPOSHIRIKI NAMI KATIKA DHIKI YANGU”. Katika maneno yanayofuata aneleza kwa nini walifanya vema kumhudumia katika dhiki yake.

            “Nanyi pia, ninyi wenyewe mnajua, enyi Wafilipi, ya kuwa   katika mwanzo wa Injili, nilipotoka Makedonia, hakuna   kanisa lingine lililoshirikiana nami katika habari hii ya               KUTOA NA KUPOKEA, ila ninyi peke yenu. Kwa kuwa  hata huko Thesalonike mliniletea msaada kwa mahitaji  yangu, wala si mara moja. Si kwamba nakitamani kile kipawa, bali NAYATAMANI MAZAO YANAYOZIDI KUWA MENGI, katika HESABU YENU” (Wafilipi 4:15 – 17).

            Ni wazi kabisa ya kuwa kwa sababu ya kushiriki katika habari ya KUTOA NA KUPOKEA – Wafilipi hawakufilisika wala kupungukiwa bali MAZAO YALIZIDI KUWA MENGI KATIKA HESABU YAO. Huyu Mungu aliyewafanikisha Wafilipi, ndiye atakayekufanikisha wewe na kuongeza mazao mengi katika habari hii ya KUTOA na KUPOKEA.

            Kumbuka siku zote kuishi kwa kuitumia na kutegemea tabia ya Mungu iliyo ndani yako katika Kristo. Tabia hii itakusaidia kutoa na kutegemea kupokea – kupanda na kutegemea kuvuna. Imeandikwa hivi

            “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa – sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu” (Luka 6:38)

 

SADAKA NA WOKOVU

             “Palikuwa na mtu Kaisaria jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu SADAKA NYINGI, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na SADAKA ZAKO zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro. Yeye ni mgeni wa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi, ambaye nyumba yake iko pwani; ATAKUAMBIA YAKUPASAYO KUTENDA” (Matendo ya Mitume 10:1 – 6).

            Tabia hii ya Kornelio ya kuwa mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, na pia tabia ya utoaji wa sadaka na kumwomba Mungu daima, inaonyesha wazi kuwa Kornelio alimpenda Mungu sana na alikuwa anatafuta namna yakukubalika mbele zake na namna ya kumpendeza Yeye.

            Tungezungumza kwa lugha nyepesi zaidi, ni kwamba alitaka kwa MATENDO YAKE aende mbinguni na kuurithi Uzima wa Milele baada ya kufa kwake . Kwa kifupi alimtafuta Mungu kwa njia ya Matendo.

            Hii ina maana ya kuwa Kornelio alitaka kuvuna  baraka za Agano Jipya katika damu Yesu, wa kutumia njia za kupendeza Mungu zilizomo katika Agano la Kale.

            Tena ingawa yeye hakuwa Myahudi kwa kuzaliwa, alitaka sana kuvuna baraka ambazo Mungu aliahidi juu ya Wayahudi.

            Mpaka hivi leo kuna watu wengi wanataka kuvuna baraka toka kwa Mungu bila kutumia utaratibu aliouweka Mungu wa kuzipokea. Ni vigumu sana kupokea ahadi za Mungu nje ya mpango wake.

            Huwezi kupokea ahadi za agano la kale kwa kutumia mbini za agano la kale na huku sasa hivi tumo katika kipindi cha agano jipya.

            Baraka zote zilizomo katika agano la kale aliahidiwa Ibrahimu na uzao wake MILELE. Soma mwenyewe Mwanzo sura ya 17 na 22. Kwa hiyo ukitaka kupokea baraka za agano la kale lililofungwa kati ya Mungu na Ibrahimu, inabidi uwe mzao au mtoto wa Ibrahim. - Kornelio hakufahamu hili; hata leo hii wengi hawafahamu.

            Baraka zote zilizomo katika agano jipya zimeahidiwa wale walio ndani ya Kristo – waliotoa maisha yao kwa Yesu kama vile Yesu Kristo alivyotoa maisha yake kwa ajili yao.

            Ni vigumu kupokea baraka za ahadi za agano la kale na zile za agano jipya NJE YA YESU KRISTO. Imeandikwa hivi katika Wagalatia 3:13,14,29;

“Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, baraka ya Ibrahimu IWAFIKILIE MATAIFA KATIKA YESU KRISTO, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani…… Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi. "

  Ndiyo maana Mungu alimtuma Malaika wake ili amwambie Kornelio kuwa amwite Simon Petro ili awaeleze habari za Yesu Kristo – ili baraka ya Ibrahimu iwafikie na wapate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani –  SIYO KWA MATENDO PEKE YAKE.
            Jambo ambalo Mungu alitaka Kornelio ajue na sisi pia tujue ni kuwa matendo mema, maombi na SADAKA bila “kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani” yaani kuzaliwa mara ya pili kwa Roho au kuokoka – haitoshi  kumpendeza Mungu, wala kukubalika mbele zake au kuhesabiwa haki.

            Ndiyo maana Yesu Kristo alimwambia Nikodemo, yule Farisayo kuwa “Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu ….. Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, HAMNA BUDI kuzaliwa mara ya   pili”(Yohana 3:3,7).

            Haya maneno “Hamna Budi” maana yake ni “lazima” kwa hiyo Yesu Kristo alikuwa anasema “…… LAZIMA kuzaliwa mara ya pili”.

            Yesu Kristo alikuwa anasisitiza kwa Nikodemo, na hata kwetu sote tunaotaka kuurithi ufalme wa Mungu, kuwa hakuna njia nyingine isipokuwa LAZIMA kuzaliwa mara ya pili kwa Roho (au kwa maneno mengine) LAZIMA Kuokoka!

IMANI NA MATENDO

                  Matendo peke yake hayatoshi kukupa ufalme wa Mungu. Kuna watu wengi sana ambao ni waaminifu sana katika kusali na kumtolea Mungu sadaka, lakini hawakubaliani na jambo kuokoka. Wanaona kuwa wao tayari wameokoka kwa sababu tu wanasali, wanatoa sadaka na kujitahidi kuishi katika matendo mema. Hebu soma   maneno ya mistari hii uone yanavyopingana na msimamo huu;

“Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; WALA SI KWA MATENDO, mtu awaye yote asije akajisifu” (Waefeso 2:8,9)

          Tunaokoka kwa njia ya imani itendayo kazi katika Yesu Kristo, “Wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu”. Matendo yana faida zaidi kwa mtu baada ya kuokoka. Na pia imani bila matendo, imani hiyo imekufa nafsini mwake. Biblia inasema hivi:

           “Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo? Je! ile imani yaweza kumwokoa?…. Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake. Lakini mtu atasema, wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha IMANI YANGU KWA NJIA YA MATENDO YANGU …….. Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa” (Yakobo 2:14,17,18,26).

                  Jambo ambalo Yakobo alikuwa anasisitiza hapa ni kutaka kuwaonya watu kuwa kusema wewe ni mkristo na huku matendo yako hayalingani na ushuhuda wa mdomo wako ni bure. Wokovu uonekane katika maisha yetu kila siku – la sivyo imani tuliyo nayo inakosa kuzaa matunda ya uzima wa milele. Ndiyo maana Yesu Kristo aliwahi kuzungumza juu ya kukatwa kwa tawi (Mkristo) lisilo zaa, soma Yohana 15:1-8 ili upate picha zaidi juu ya jambo hili.

CHUKUA HATUA LEO

          Malaika alimwambia Kornelio atume watu wakamwite Simoni aitwaye Petro ili AMWAMBIE YAMPASAYO KUTENDA. Mungu kwa uweza wa Roho wake Mtakatifu amekuletea maneno haya mkononi mwako ili UFAHAMU YAKUPASAYO KUTENDA.

          Kama hujaokoka na unadhani unaweza kuokoka kwa kutoa sadaka nyingi NAKUSHAURI KWA JINA LA YESU KRISTO WA NAZARETI uombe sala hii kwa sauti, ili utubu na kumpa Yesu Kristo maisha yako leo. HALAFU endelea kutoa sadaka nyingi ukiwa ndani ya Yesu Kristo.

          Omba sala hii kwa sauti; “Mungu Baba, unisamehe dhambi zangu zote nilizokukosea katika maisha yangu. Ninatubu kwako. Nitakase kwa damu ya Yesu Kristo. Bwana Yesu Kristo nimefungua moyo wangu nakukaribisha uingie ndani yangu, kwa uwezo wa Roho wako. Uwe Bwana na Mwokozi wa maisha yangu – sasa na hata milele. Asante kwa kunisamehe dhambi na kuniokoa. Amina”.

          Ikiwa umeisema sala hii kwa uaminifu, basi umefanyika kiumbe kipya – umezaliwa mara ya pili na Mungu hakumbuki dhambi zako tena. Soma 2Wakorintho 5:17, Waebrania 8:12. Karibu sana katika ufalme wa Mungu kwa jina la Yesu Kristo!

          Hili ndilo lililotokea kwa Kornelio na jamaa yake, Simoni Petro alipofika kwao aliwaambia habari za Yesu Kristo – walisikia maneno hayo wakamwamini Yesu na kujazwa na nguvu za Roho Mtakatifu wakati huo huo.

 

 

NATOA LAKINI SIPOKEI – NIFANYEJE?

            Kuna wakati fulani, mtu mmoja alinifuata baada ya kipindi nilichokuwa nafundisha Neno la Mungu juu ya utoaji, na akaniuliza hivi; “Kwa nini mimi nimekuwa natoa zaka na sadaka nyingi lakini sipokei? Hata miradi niliyo nayo haifanikiwi nilivyokusudia – ni kwa nini iwe hivyo.

            Inawezekana na wewe unayesoma ujumbe huu sasa una maswali kama haya. Hayo ni maswali ya msingi na ni muhimu tupate ufumbuzi wake. Hata mkulima ambaye alipanda mbegu katika shamba, na asipate kitu au apate mavuno machache, atajiuliza maswali kumetokea kitu gani.

           Tukumbuke ya kuwa si mapenzi ya Mungu tuwe maskini – tuwe na hali ngumu kimavazi, chakula na kiafya. Pia, tukumbuke ya kuwa ni tabia ya kiuungu mtu kutoa na kutegemea kupokea. Ingawa si lazima upate toka kwa mtu huyo huyo uliyempa, - maana Mungu anaweza kumgusa mtu mwingine akupe – lakini utaratibu wa Mungu unabaki pale pale, ukitoa tegemea kupokea.

            Ni kitu gani kinasababisha mtu asipokee na huku amekuwa akijitahidi kutoa? Biblia inatuambia ya kuwa tukiwa waaminifu katika utoaji, Mungu atatumwagia baraka, “hata isiwepo nafasi ya kutosha ya kuziweka” – Je! umewahi kumsikia mkristo yo yote akisema amepata baraka nyingi mno hata amekosa mahali pa kuziweka?

Sababu zifuatazo zitatusaidia kujua ni kwa nini hatufanikiwi katika utoaji wetu – na hata hatupokei kama tulivyotegemea na kutarajia;

1. KUVUNJA MIIKO AU UTARATIBU WA UTOAJI

            Kila jambo lina utaratibu wake – usipoufuata usitegemee mavuno mazuri. Kilimo cha mahindi kina utaratibu wake wa upandaji na palizi tofauti na kilimo cha ngano au cha kabichi. Ndiyo maana wataalamu wa kilimo, walianzisha kampeni za kuwafundisha wakulima juu ya “kilimo cha kisasa” ili kiwasaidie wakulima kupata “mavuno” zaidi toka katika mashamba yao.

        Hata katika “kupanda na kuvuna” au “kutoa na kupokea” katika mambo ya Mungu kuna utaratibu wake. Ukienda kinyume na utaratibu huo, usitegemee mavuno ya kuridhisha toka katika utoaji wako 

Kwa mfano hebu soma na kutafakari maneno haya yafuatayo:

            “Lakini nasema neno hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu na atende kama ilivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana   Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu” (2Wakorintho 9:6,7).

“….wala si kama kitu kitolewacho kwa unyimivu” (2Wakorintho 9:5).

          Utaona katika mistari hiyo Mungu ametueleza kwa kiasi fulani utaratibu ambao anataka ufuatwe mtu akitaka kuvuna katika utoaji wake. Je! unafuata utaratibu huu katika utoaji wako?

             Utaratibu huoni huu; utoaji wako uwe si haba (au kidogo) bali uwe kwa ukarimu. Ukitoa kidogoutapata kidogo – bali ukitoa vingi utapata vingi. Ndiyo maanaimeandikwa;

            “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. KWA KUWA KIPIMO KILE KILE MPIMACHO NDICHO MTAKACHOPIMIWA” (Luka 6:38)

          Kama unataka kutoa sadaka tu “ kama ulivyokusudia moyoni mwako”. Kama ulikusudia kutoa shilingi 100/= toa shilingi 100/=. Fanya hivi siku zote na utafanikiwa.

             Tena, utoajiunatakiwa ufanyike “si kwa huzuni; wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeyeatoaye kwa moyo wa ukunjufu “… na walasi kwa unyimivu”.

          Michango mingi iliyomo makanisani siku hizi wakati mwingine inafanyika kwa kulazimishana.Mtu anatakiwa atoe kwa kupenda kwake toka moyoni mwake – SI KWA LAZIMA.Kumlazimisha mtu kutoa ni kwenda kinyume cha utaratibu wa utoaji.

             Wakristo wengiwamekosa baraka au mafanikio katika utoaji kwa sababu wanatoa huku WANAHUZUNIKAAU WANALALAMIKA! Wengi wanawanung’unikiaviongozi wa makanisa yao kuwa wanatumiafedha au vitu vibaya. Kama una wasiwasi na matumizi ya matoleo yako – yaombeekwa Mungu ayalinde yatumike kwa utukufu wake kuliko kulalamika.

          Wengine wanahuzunika na kulalamika kuwa michango imezidi. Je! umewahi kumsikia mkulima akihuzunika au kulalamika kwa kuwa ameongezewa shamba la kulima na kupanda? Hakuna. Mkulima halalamiki bali anafurahi kwa kuwa amepata eneo kubwa zaidi la kupanda umeongezewa eneo la KUPANDA ili AVUNE ZAIDI. Ni eneo la kukusaidia kutoa zaidi ili UPOKEE ZAIDI!

2. IBILISI AMEZUIA BARAKA ZAKO;

           Kati ya baraka ambazo zinapatikana kutokana na mtu kuwa mwaminifu katika utoaji wa zaka (fungu la kumi) na dhabihu (matoleo mbalimbali) na kuzidiwa wakati wa matatizo, Mungu alisema hivi;

         “Nami kwa ajili yenu nitamkemea yeye alaye, wala hataharibu mazao ya ardhi yenu; wala mzabibu wenu hautapukutisha matunda yake kabla ya wakati wake katika mashamba ….” (Malaki 3:11).

            Ni wazi kuwa aliye nyuma ya kuharibika kwa mazao shambani au biashara ni yule ‘alaye’ ambaye ni Ibilisi. (Hii ni kama mkulima au mfanya biashara amefanya anachotakiwa kukifanya kilicho ndani ya uwezo wake).

            Kinyume cha jambo hili ni kwamba usipokuwa mwaminifu kutoa fungu la kumi toka katika mazao ya shamba lako, usitegemee Mungu akupiganie wakati mharibu anapoingilia mimea yako na kuiharibu. Vile vile usipokuwa mwaminifu kutoa fungu la kumi toka katika mapato ya biashara yako, usitegemee Mungu akusaidie wakati mharibu anapoingilia biashara yako na kuiharibu.

            Inawezekana unatoa sadaka, na huoni baraka zozote zinazotokana na kutoa kwako – hebu angalia na jichunguze kama umekuwa mwaminifu katika kutoa ZAKA KAMILI. Kwa mfano kama fungu la kumi la pato lako ni shilingi 2,000 – toa zaka kamili yaani shilingi 200/=. Usitoe pungufu ya hiyo maana haitakuwa zaka KAMILI.

           Ikiwa umekuwa mwaminifu katika kutoa Zaka kamili na dhabihu halafu huoni matokeo yake basi, tumia mamlaka ya Jina la Yesu Kristo – mfunge na kumkemea ibilisi ambaye ndiye mharibu wa mali yako aondoe mikono yake juu ya mali yako.

 Kumbuka Yesu Kristo alisema;
            “Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lo lote utakalofunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni” (Mathayo 16:19).

    Kuna mtumishi mmoja wa Mungu ambaye anasimulia jinsi ambavyo mkulima mmoja wa pamba alivyosaidika na uwezo wa jina la Yesu Kristo.

    Huyo Mkulima alikuwa mwaminifu katika kumtolea Mungu fungu la kumi la mapato ya shamba lake kila mwaka, na alikuwa haelewi kwa nini pamba yake ilikuwa haifunguki ingawa muda wa kufunguka na kuchanua ulikuwa umefika. Wataalamu wa kilimo cha pamba walikuja kuliangalia shamba hilo lakini hawakuweza kumsaidia mkulima huyo kutatua tatizo hilo.

    Mtumishi wa Mungu huyo alifika hapo, na alisikia habari ya mahangaiko ya mkulima huyo. Baada ya kufahamu ya kuwa mkulima huyo alikuwa mwaminifu katika kutoa fungu la kumi – alimwambia waende shambani ili waombe.

    Huyo mtumishi wa Mungu wakiwa shambani na mkulima huyo; - akimkumbusha Mungu juu ya ahadi yake ya Malaki 3:7-11. Na mwishoni akamwamuru ibilisi aondoke kwenye pamba hiyo. Mara tu baada ya kumaliza sala hiyo – pamba ilianza kufunguka na kuchanua! Bwana asifiwe sana kwa uwezo huu ulivyo wa ajabu.

        Usibaki unalalamika na kuhangaika kama vile mtu asiyejua ahadi za Mungu. Simamia haki zako ndani ya Kristo kwa kuwa mtendaji wa neno na utafanikiwa.

3. KUTOKUPANDA KATIKA UDONGO MZURI

           Utoaji ni sawasawa na upandaji. Mtu akipanda anategemea kuvuna pia. Kwa hiyo mtu akitoa anategemea kupokea.

    Mkulima yo yote akitaka mavuno mazuri toka shambani mwake kati ya vitu anavyoviangalia ni aina ya mbegu na aina ya udongo. Siku zote atapanda kwenye udongo mzuri wenye rutuba.
            Mfanya biashara siku zote anataka aweke mtaji wake katika vitu vitakavyomletea faida kibiashara na siyo hasara.
            Lakini, inasikitisha kuona kuwa inapofika wakati wa utoaji – wakristo wanatoa tu bila kuangalia kwanza “udongo mzuri” ni upi ili utoaji wao uwaletee matokeo mazuri.

    Biblia inatuambia katika mfano wa mpanzi ya kuwa mbegu zingine“…. Zikaanguka penye udongo ulio mzuri, zikazaa matunda, zikimea na kukua, na kuzaa, moja thelathini, moja sitini, na moja mia” (Mathayo 4:8).

         Je, “udongo mzuri” unaoleta faida nzuri ni upi? Sehemu za kutoa zenye matokeo au mavuno mazuri ni hizi zifuatazo;

(a)         Katika nyumba ya Mungu – kanisani ili kuendeleza kazi ya Mungu – soma Malaki 3:10-11; na Kumbukumbu ya Torati 8:18.

(b)        Kuwasaidia watumishi wa Mungu na watakatifu wake kwa vitu/mali ulizo nazo. Soma 1Wafalme 17:10-24 na 2Wakorintho 9:10-13.

(c)         Kuwasaidia maskini kwa vitu/mali ulizo nazo. Soma 2Wakorintho 9:8-9.

    Angalia upandaji wako katika utoaji – je! umepanda kwenye udongo ulio mzuri?

4.  KUKATA TAMAA

           Wagalatia 6:9 inasema hivi; “Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho”.
Tafsiri iliyo nyepesi inasema, “maana tutavuna kwa wakati wake tusipokata tamaa”.
            Wakristo wengi wanatoa lakini hawana uvumilivu. Mkulima asipokuwa mvumilivu kusubiri mazao ya shamba lake yanayokuja kwa wakati wake – hawezi kuvuna alichopanda.
            Vile vile mtoaji asiyejifunza kumvumilia Mungu ili amletee matokeo ya utoaji huo kwa WAKATI WAKE – hawezi kuvuna alichopanda.
            Mungu si mwongo! Wala ahadi zake hazijui kusema uongo. Alichoahidi atatenda. Ukitoa utapokea KWA WAKATI WAKE USIPOKATA TAMAA.
            Usianze kutafuta njia za mkato ili ufanikiwe – uwe mvumilivu ulichopanda kwenye udongo mzuri utavuna.
            Mkumbuke Ibrahimu alivyovumilia. Biblia inasema hivi;
            “Lakini akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutokuamini, bali alitiwa nguvu kwa imani, akimtukuza Mungu; huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya yale aliyoahidi” (Warumi 4:20-21).

5.KUTOA KWA MAJIVUNO NA KUTAFUTA KUSIFIWA NA WATU

            “Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni. Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili WATUKUZWE NA WATU. Amin, nawaambieni,wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri; na BABA YAKO AONAYE SIRINI ATAKUJAZI” (Mathayo 6:1- 4

 

 

 

UFANYEJE KATIKA HALI NGUMU YA UCHUMI?

Matatizo ya ugumu wa uchumi katika dunia hii siyo mapya. Tangu baada ya mwanadamu kuanguka katika dhambi – amekuwa mara kwa mara akisumbuliwa na matatizo ya uchumi. Ukisoma habari za Isaka na za Yakobo utaona jinsi hali hii ilivyojitokeza.

Lakini biblia inaeleza wazi kuwa siku hizi ni mwisho. Katika siku hizi za mwisho, biblia pia inasema wazi kabisa kuwa dunia itapita kwenye vipindi vigumu vya uchumi

Kwa Mfano: Katika Mathayo 24:7 na Ufunuo wa Yohana 6:3-6 tunaona ya kuwa katika siku hizi za mwisho kutatokea njaa – au upungufu wa chakula. Sababu ya kuja kwa njaa hiyo ni vita vitakavyokuwa vinatokea katika nchi mbalimbali. Ni wazi kabisa kuwa palipo na vita au palipo na ugomvi, panakuwa na matatizo ya ulimaji mashamba na usafiri wa kuleta chakula toka sehemu zingine. Matokeo ni hilo eneo au nchi kukosa chakula, haya mambo yaliyotabiriwa kutokea siku hizi za mwisho wa dunia.

Ukisoma katika kitabu cha Ufunuo wa Yohana sura za 17 na 18 utaona ya kuwa hali ngumu ya kibiashara imetabiriwa kutokea katika siku hizi za mwisho. Kuuza au kununua kutafanyika kwa vibali. Watu watapenda fedha sana kuliko kumpenda Mungu. Kutakuwa na uhusiano mkubwa sana kati ya utajiri na biashara na uasherati. Wafanya biashara wa siku hizi za mwisho watakuwa na sehemu kubwa katika utawala wa miji au vijiji wanavyokaa – hata wakati mwingine katika maongozi ya nchi au mataifa mbalimbali.

Matokeo ya hali namna hii inawafanya watu watafute njia au mbinu za kuweza kuishi katika vipindi vya namna hiyo. Lakini ni wazi kuwa si mbinu zote au njia zote ambazo wanadamu wanazitumia katika kuishi wakati wa hali ngumu ya uchumi zinampendeza Mungu.

Kunapotokea hali ngumu ya uchumi, tabia za watu zinabadilika. Mara kwa mara mambo yafuatayo hutokea;

Kubana matumizi Kununua vitu kwa wingi na kuvirundika Uchoyo – kupunguza tabia ya utoaji na ukarimu Watu huacha kumtumikia Mungu na badala yake mtu huitumikia mali Rushwa, wizi na dhuluma huwa ni vitu vya kawaida Miradi ya kila namna huibuka kuanzia kwa watoto hadi watu wazima.

Jambo linalowafanya watu wawe na tabia hizi, ni lile la kutaka kutafuta namna ya kuishi katika kipindi kigumu cha uchumi. Je!mkristo afanye nini ili aishi katika kipindi hiki kigumu cha uchumi bila kufanya mambo yatakayomkosea Mungu?

Wakristo wengine wamefika mahali pa kuhalalisha miradi ya kuwapatia fedha ambayo ni kinyume na ushuhuda wa kikristo – Je! hii ni sawa?

Wengine wamefika hata mahali pa kufunga nira na wasioamini (wasio wakristo) KWA JINSI ISIYO SAWASAWA (yaani isiyokubalika) na neno la Mungu ili waweze kupata fedha kutokana na mradi wanaofanya pamoja. IKO "jinsi iliyo sawasawa" na utaifahamu ikiwa utakuwa mtendaji wa neno la Mungu.

Wakristo si wa ulimwengu huu

Ndugu au Dada unayesoma sasa mambo haya – sikiliza! Sisi kama wakristo si wa ulimwengu huu ingawa tunaishi hapa ulimwenguni. Fahamu na kumbuka hili kila wakati. Yesu Kristo alisema hivi;

"Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo naliwatuma hao ulimwenguni" (Yohana 17:14-18).

Je! unafikiri Yesu Kristo anaweza kututuma hapa duniani bila kutuandaa kuishi kiushindi katika majaribu yaliyomo ndani yake na hali ngumu ya uchumi?

Je! unadhani Yesu Kristo anaweza kukuokoa halafu asikutunze kiuchumi katika maisha mapya ya wokovu? Nafahamu kuna wakristo wengi walioanguka kiroho kwa sababu ya kutafuta njia za kujisaidia kimaisha.

Biblia inatuambia ya kuwa Yesu Kristo huwalisha na kuwatunza watu wake ili ajiletee kanisa (wakristo) walio watakatifu. Soma Waefeso 5:25-33.

Katika vipindi vyote vya matatizo ya uchumi, Mungu ameweza kuwalisha na kuwatunza watu wake. Wamekula na kuvaa na kulala ndani ya mpango wake bila kumkosea.

Katika siku hizi za mwisho, Kristo anazungumza na kulikumbusha kanisa (wakristo) juu ya njia au mbinu za kuchukua wakati wa hali ngumu ya uchumi mahali walipo.

Mashauri muhimu ya kufanya

Fuata maongozi ya Mungu na siyo ya dunia: Ni rahisi sana kusikia na kufuata ushauri wa wanadamu kuliko ushauri wa Mungu hasa mtu anapobanwa na shida. Lakini kwa mkristo nakushauri siku zote kuwe na shida au kusiwe na shida, fuata ushauri wa Mungu kama vile anavyokuongoza kwa Roho Mtakatifu katika neno lake. Tuangalie jinsi Isaka alivyofanya alipokumbwa na hali ya njaa.

"Ikawa njaa katika nchi hiyo, mbali na njaa ile ya kwanza iliyokuwa siku za Ibrahimu. Isaka akamwendea Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, huko Gerari. Bwana akamtokea, akasema, usishuke kwenda Misri, kaa katika nchi nitakayokuambia …. Nami nitakuwa pamoja nawe, na kukubariki …" (Mwanzo 25:1-3).

Njaa ilipotokea huko Gerari, watu walianza kuondoka huko na kwenda Misri, ili kutafuta chakula. Ni wazi ya kuwa hata Isaka alitaka kufanya hivyo. Bwana akamzuia akamwambia asiondoke bali akae katika nchi aliyomwambia na katika nchi hiyo atakuwa pamoja naye na kumbariki au kumfanikisha.

Nataka kukukumbusha ya kuwa baraka za Mungu kwetu hazitegemei jinsi hali ya hewa na uchumi wa dunia hii unavyokwenda bali zinategemea NENO LA KRISTO.

Isaka akatii, hakuondoka bali alibaki katika nchi hiyo ambayo watu walikuwa hawapati chakula wakilima.

"Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, Bwana akambariki" (Mwanzo 26:12).

Siku zote kaa na kufanya kazi mahali ambapo Mungu amekuongoza kukaa. Usihame mahali au kuacha kazi, bila uongozi wa Mungu. Kufanikiwa kwako hakutegemei mipango yako bali kunategemea mpango wa Mungu.

Ukiwa ndani ya Kristo utafanikiwa mahali po pote pale ambapo Mungu atakapokuweka hata kama mazingira yake kibinadamu si mazuri kwa kufanikiwa. Ukiwa ndani ya Kristo, "Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani … utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa utokapo …. Bwana ataiamuru baraka ije juu yako katika ghala zako, na mambo yote utakayotia mkono wako; naye atakubarikia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako" (Kumbukumbu ya Torati 28:3,6,8).

Endelea kutoa hata wakati wa upungufu

Katika hali ya kibinadamu upungufu unapotokea mahali watu wanabana matumizi – na hali ya ukarimu na utoaji huwa inafifia sana hata wakati mwingine kupokea kabisa. Wakristo wengi pia wamekumbwa na hali hii – wanasema wamepunguza utoaji kwa kuwa wamepungukiwa na hali ya uchumi ni ngumu. Je! hii ni sawa?

Wakati wa ukame ulipotokea wakati wa maisha ya Nabii Eliya Mtishbi; Bwana alimwambia Eliya, "Ondoka, uende Sarepta, ulio mji wa Sidoni, ukae huko. Tazama, nimemwagiza mwanamke mjane wa huko akulishe" (1Wafalme 17:9).

Unakumbuka jinsi yule mama alivyojitetea wakati Eliya alipofika kwake ili alishwe? Yule mama alijitetea kama watu wengine wanavyojitetea siku hizi wakitakiwa kutoa au kuchanga walivyo navyo kwa ajili ya kazi ya Mungu. Naye yule Mjane akasema;

"Kama Bwana, Mungu wako, aishivyo, sina mkate, ila konzi ya unga katika pipa, na mafuta kidogo katika chupa; nami ninaokota kuni mbili ili niingie nijipikie nafsi yangu na mwanangu, tule tukafe" (1Wafalme 17:12).

Kwa jinsi ya kibinadamu, Eliya angeweza kumwonea huruma yule mama, asile chakula chake; na aondoke na aende kwa matajiri wa siku zile kupata chakula. Lakini Eliya hakufanya hivyo- bali ALITII MAAGIZO YA MUNGU. Eliya akamwambia yule mjane hivi;

"Usiogope;enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie KWANZA mkate mdogo ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao" (1Wafalme 17:13).

Ndivyo yule mama alivyofanya – alimpa KWANZA MUNGU kwa kupitia mtumishi wake. Mungu akambariki yule mama kwa ukarimu na utoaji wake wakati alipokuwa na upungufu. "Lile pipa la unga HALIKUPUNGUKA, wala ile chupa ya mafuta HAIKUISHA sawasawa na NENO LA BWANA alilolinena kwa kinywa cha Eliya" (1Wafalme 17:16).

Katika hali ya upungufu ulionao, usiwe mchoyo bali endelea kumtolea Mungu, naye atakubariki na kukufanikisha. Na hii itaonyesha ni kwa kiasi gani unamtegemea Mungu wako na Neno lake.

Lazima ufahamu ya kuwa Yesu Kristo anaangalia sana jinsi tutoavyo. Siku moja akiangalia jinsi watu watoavyo fedha; "Akawaita wanafunzi wake, akawaambia, Amin, nawambia, Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la Hazina; maana hao wote walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia" (Marko 12:43-44). Soma na kuyatafakari tena maneno hayo ya Yesu Kristo, halafu jiangalie jinsi utoavyo. Huyu mjane hakuwa na mali ya kutosha alikuwa maskini, lakini bado aliendelea kumtolea Mungu! Je wewe una la kujitetea katika kutomtolea Mungu wakati wa upungufu wako?

Weka hazina yako mbinguni

Yesu Kristo alisema;"Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo,na wezi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wezi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako" (Mathayo 6:19 – 21).

Utoaji wako utaonyesha kama moyo wako uko kwa Yesu au unaitegemea dunia. Moyo wako ukimtegemea sana Yesu, utatoa zaidi kwa ajili ya kazi ya Mungu kuliko mahali pengine. Mkristo anapopoa kiroho, utoaji wake HASA kwa kazi ya kuhubiri injili nao unapungua. Hata hivyo Biblia inatuambia katika siku za mwisho upendo wa wengi utapoa.

Mtolee Mungu zaka na dhabihu (matoleo) bila kuchoka, nawe utakuwa umeweka hazina yako mbinguni – mikononi mwa Mungu – ambamo wezi hawawezi kukuibia. Naye Bwana atakurudishia mara nyingi zaidi. Mradi mzuri na wenye uhakika wa mavuno kwa Mungu na kwako wakati wa hali ngumu ya uchumi ni mradi wa kuhubiri injili. Kwa hiyo siku zote hakikisha umeweka kiasi fulani katika mradi wa kuhubiri injili.

Dumu katika maombi

Hili ni muhimu sana. Kwa kuwa wakristo wengi wakiwa katika hali ya ugumu wa maisha na uchumi, wanapoa katika maombi – na wanakumbwa na majaribu ambayo mara nyingi yanachafua ushuhuda wao. Soma Luka 21:36, Mathayo 24:42 – 51 na Mathayo 26:41. Kwa hiyo dumu katika maombi, usikate tamaa, hata wakati wa hali ngumu kiuchumi kwa upande wako – bado zidi kudumu katika maombi.

JE! MAFANIKIO YAKO
KIFEDHA YANA MATATIZO?

            Mwaka 1997 tulipokea barua na simu nyingi toka kwa watu wa Mungu mbalimbali wakihitaji maombi kwa ajili ya matatizo yaliyokuwa yanawasumbua katika maeneo ya kifedha. Wengine biashara na kazi zao vilikuwa haviendi vizuri - nakadhalika.
            Tulikaa na jambo hili katika maombi. Tarehe 24 Septemba 1997 saa kumi na nusu asubuhi tukiwa katika maombi Bwana Yesu alisema nasi katika mioyo yetu ujumbe ufuatao ambao tunaamini utakusaidia hata wewe. Bwana Yesu alituambia hivi:

·         roho ya mpinga Kristo ndiyo iliyoshambulia mafanikio ya kifedha katika watu  wangu,

·         Imeelekeza mashambulizi katika mafanikio ya roho zao (na nafsi zao) maana nimesema mtafanikiwa katika mambo yote kwa kadri roho zenu zifanikiwavyo,

·         Kufanikikiwa kwa roho zenu kunategemea kufanikiwa kwa nafsi zenu. Mtafanikiwa katika roho zenu kwa kadri nafsi zenu zifanikiwavyo, na matokeo yataonekana katika mambo yote

·         Nafsi zenu zifanikiwavyo zinategemea utendaji wenu wa Neno langu. Ikiwa utendaji wenu wa Neno ukiwa hafifu, na kufanikiwa kwa nafsi zenu kunakuwa hafifu. Kufanikiwa kwa nafsi zenu kukuwa hafifu na kufanikiwa kwa roho zenu kunakuwa hafifu, kwa hiyo kufanikiwa katika mambo yote kunakuwa hafifu pia.

·         Ndiyo maana nasema roho ya mpinga Kristo imeelekeza mashambulizi yake katika kupinga, kuzuia, na kuchelewesha mafanikio yenu katika roho na nafsi zenu.

·         Lakini mnaweza kushinda kwa kusimama katika Neno langu ambalo ni upanga wa Roho mikononi mwenu.

·         Nimesema katika Yoshua 1:8 ya kuwa mtafanikiwa ikiwa mambo matatu yatafanyika juu ya Neno langu:
(a) Lisiondoke kinywani mwenu 
(b) Mlitafakari wakati wote
(c) Na kudumu kulitenda

·         Sasa angalia mmesimamaje katika maeneo hayo matatu. Maana hizo ni mbinu za kulitumia Neno langu kama silaha ya kumshinda adui

·         Mkisimama katika Neno langu ninavyotaka mtavuna mafanikio sana kwa wakati wangu msipozimia na kukata tamaa katika mioyo yenu.

·         roho ya mpinga Kristo inawakatisha tamaa kwa kuwaangaliza matokeo ya upungufu mlionao badala ya kuangalia ahadi zangu na matokeo yake.

·         Kwa kadri mnavyoangalia matokeo ya upungufu mlionao, ndivyo mnavyozidi kutafakari juu ya upungufu mlionao. Kwa kadri mnavyozidi kutafakari juu ya upungufu mlionao, ndivyo mnavyozidi kukiri na kushuhudia upungufu mlionao na matokeo yake.

·         Kumbuka mnayafunga mafanikio yenu kwa maneno ya vinywa vyenu yanayotoka katika nafsi zisizotafakari ahadi zangu na matokeo yake.

·         Mimi si mtu hata niseme uongo. Nililolisema katika Neno langu nimesema nitalitimiliza. Napenda kufanikiwa kwenu kuliko nyinyi mnavyopenda kufanikiwa kwa watoto wenu. Msikubali adui ayumbishe macho yenu na mioyo yenu isione uaminifu wangu.

·         Mkisimama katika neno langu na kupigana hivyo vita vizuri vya imani mlivyo navyo;
- mtashangilia ushindi wakati kuta hazijaanguka bado,
- mtatangaza ushindi wakati bado upinzani wa adui umesimama,
- mtaona mafanikio wakati bado mmezungukwa na upungufu,

·         Kumbuka neno langu linatangaza ushindi katika roho kwanza kabla ya haujaonekana kwa nje. Ndicho kilimchomsaidia Ibrahimu wakati anasubiri mtoto wake. Na ndicho kilichonisaidia na mimi pale masalabani - nilishangilia ushindi dhidi ya adui hata kabla sijafufuka. Daudi naye aliuona ushindi wakati bado Goliati amesimama mbele yake.

            Kila mtu atakuja kwangu na kuuliza nimpe Neno la kusimamia katika vita alivyo nayo. Hamuwezi kushinda pasipo Neno.

            Haya ndiyo machache tuliyoyapokea kutoka kwa Bwana Yesu tulipofanya maombi ya kuuliza kwa nini watu wengi wa Mungu wamekuwa hawafanikiwi vizuri katika eneo la fedha. Ingawa Bwana alisema nasi mwaka 1997 tunaamini bado ujumbe una nguvu ndani yake ya kukusaidia. Tafakari maneno ya ujumbe huu, weka katika matendo yaliyomo - na Mungu atakusaidia!

            Ahsante,

Christopher na Diana Mwakasege